Nameless afichua mambo muhimu ambayo babake aliwaambia akitimiza miaka 88

Nameless alizungumza kuhusu jinsi baba yake anavyojivunia kuwa na watoto ambao hawana ugomvi wa kindugu

Muhtasari

•Mzee Joshua Mathenge alitimiza miaka 88 wikendi na mwanamuziki huyo alitumia fursa hiyo kusherehekea afya njema ya wazazi wake.

•Baba huyo wa watoto watatu pia alifunguka kuhusu shauri muhimu ambalo baba yake aliwapa kuhusu umuhimu wa kukosoana.

Mwanamuziki Nameless pamoja na wazazi wake na ndugu zake
Image: FACEBOOK// NAMELESS

Siku ya Jumapili, mwimbaji mkongwe wa Kenya David Mathenge almaarufu Nameless alikutana na ndugu zake nyumbani kwa wazazi wao kusherehekea siku ya kuzaliwa ya baba yao.

Mzee Joshua Mathenge alitimiza miaka themanini na minane wikendi na mwanamuziki huyo alitumia fursa hiyo kusherehekea afya njema ya wazazi wake.

Mume huyo wa Wahu Kagwi alizungumza kuhusu jinsi baba yake anavyojivunia kuwa na watoto ambao hawana ugomvi wa kindugu.

"Tunajumuika na baba katika siku yake ya kuzaliwa ya 88 na hatukuweza kujizuia ila kushukuru kwa afya ya mama na baba!!," Nameless alisema kupitia ukurasa wake wa Facebook.

Aliambatanisha taarifa hiyo na picha nzuri zinazomuonyesha yeye, wazazi wake na ndugu zake wakiwa katika nyakati za furaha walipokuwa wakisherehekea siku ya kuzaliwa ya Bw Mathenge.

“Baba alituambia jambo ambalo nitashika moyoni mwangu. Alisema wakati mwingine yeye hukaa na kutazama kila mmoja wa watoto wake na haamini kwamba alibarikiwa na watoto wazuri ambao hushikamana kila wakati! Hilo lilitufanya tujisikie vizuri sana!😊😊🙏🏿🙏🏿," alisema Nameless.

Baba huyo wa watoto watatu pia alifunguka kuhusu shauri muhimu ambalo baba yake aliwapa kuhusu umuhimu wa kukosoana.

"Pia alituambia tukumbuke kila wakati kuwa hatuwezi kujua kila kitu na kuwa sawa kwa kusahihishwa na pia kuwa huru kusahihishana ikiwa tunafikiria kuwa tunahitaji. Ukuaji ni muhimu katika uhusiano wowote!” aliandika.

Aliongeza, "Ilikuwa siku maalum iliyotimizwa kwetu. Heri ya kuzaliwa Baba. Wewe ni MWANAUME! 🙏🏿”

Wazazi wa mwimbaji Nameless, Mzee Joshua Mathenge na Eunice wote bado wako hai. Wamekuwa pamoja katika ndoa kwa takriban miongo sita.