Zaidi ya watu 40 wapoteza maisha baada ya bwawa kupasua Mai Mahiu

Makumi ya watu wameuawa baada ya bwawa kuvunja kingo zake katika eneo la Mai Mahiu.

Muhtasari

•Gavana Susan Kihika pia alithibitisha vifo hivyo kwa shirika la habari la AFP, na kuongeza kuwa idadi hiyo inaweza kuongezeka.

Image: HISANI

Makumi ya watu wameuawa baada ya bwawa kuvunja kingo zake katika eneo la Mai Mahiu nchini Kenya, kaskazini mwa mji mkuu, Nairobi, Shirika la Msalaba Mwekundu la Kenya limeithibitishia BBC.

Gavana wa eneo hilo Susan Kihika pia alithibitisha vifo hivyo kwa shirika la habari la AFP, na kuongeza kuwa idadi hiyo inaweza kuongezeka.

Maji yalitiririka na kusomba nyumba na magari kadhaa katika kijiji cha Kamuchiri, kufuatia mvua kubwa ambayo imekuwa ikinyesha maeneo kadhaa nchini humo.

Vikosi vya uokoaji vinachimba matope kutafuta manusura, vyombo vya habari vya eneo hilo vilisema, na kuonya kwamba idadi ya vifo inaweza kuongezeka kwa kiasi kikubwa.

Mvua hiyo ilipasua barabara kuu kutoka Nairobi kuelekea Mai Mahiu baada ya mawe makubwa, matope na magogo kuziba eneo hilo.

Mapema Jumatatu, Shirika la Msalaba Mwekundu la Kenya lilisema limewapeleka watu kadhaa katika kituo cha afya huko Mai Mahiu kutokana na mafuriko.

Vifo vya hivi punde vinafanya idadi ya watu kutokana na mvua kubwa na mafuriko nchini tangu mwezi uliopita kuongezeka hadi zaidi ya 100.