Shirika la ndege la Kenya Airways lasitisha safari za ndege kuelekea mji mkuu wa DR Congo - kunani?

KQ ilisitisha safari za ndege kuelekea Kinshasa kwa sababu ya kuzuiliwa kwa wafanyikazi wawili na majasusi wa kijeshi.

Muhtasari

• Afisa mkuu mtendaji wa KQ alisema "mzigo huo haukubebwa au kukubaliwa na KQ kutokana na kutokamilika kwa nyaraka".

Ndege ya Kenya Airways
Image: MAKTABA

Shirika la ndege la Kenya Airways (KQ) linasema kuwa limesitisha safari za ndege kuelekea mji mkuu wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo Kinshasa kwa sababu ya kuzuiliwa "kinyume na sheria" kwa wafanyikazi wawili na ujasusi wa kijeshi.

KQ ilitoa tangazo hilo Jumatatu katika taarifa kwenye X, ambayo zamani ilikuwa Twitter, na kusema "hawawezi kuedeleza safari za ndege bila wafanyikazi hao".Walisema kusimamishwa kwa safari hizo kutaanza Jumanne.

Tarehe 19 Aprili, wafanyakazi wawili wa KQ waliwekwa chini ya ulinzi na Uchunguzi wa Kijeshi (DEMIAP) kwa sababu ya madai ya "kukosa nyaraka za forodha za mizigo ya thamani", kulingana na shirika hilo la ndege.

Lakini afisa mkuu mtendaji wa KQ alisema "mzigo huo haukubebwa au kukubaliwa na KQ kutokana na kutokamilika kwa nyaraka".

Wakati wa kukamatwa kwao , simu za wafanyikazi hao wawili zilichukuliwa na kuzuiliwa hadi Aprili 23 wakati maafisa wa Ubalozi na timu ya KQ waliruhusiwa kuwatembelea.

Kampuni ya ndege iliwahimiza wanajeshi wa Kongo kuwaachilia wafanyikazi wa KQ kwa familia zao.

Serikali ya DR Congo haijatoa tamko lolote.