logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Mlinzi afikishwa mahakamani kwa kupapasa matiti na makalio ya mhudumu wa hoteli

Mwanamke huyo aliwaambia polisi kwamba mshtakiwa alianza kummiminia maneno ya sifa akisema ni mkarimu, mrembo na ana umbo zuri huku akianza kumshikashika matako kwa mikono yake.

image
na

Burudani15 January 2022 - 04:57

Muhtasari


•Karatasi ya mashtaka inasema mshtakiwa alimgusa JPN matako kwa mikono yake kinyume na kanuni za adhabu.

•Mshtakiwa alikana kutenda kosa hilo mbele ya Hakimu mkuu wa Kibera Derrick Kuto na kuachiliwa kwa bondi ya Sh300, 000

Dainon Lempirdaany katika mahakama ya Kibera

Mlinzi mmoja anayedaiwa kumfanyia mwanamke mmoja kitendo kisicho cha heshima katika mkahawa aliokuwa akiulinda alifikishwa katika mahakama ya Kibera Jumatano na kufunguliwa mashtaka.

Kulingana na karatasi ya mashtaka,Dainon Lempirdaany, alitenda kosa hilo mnamo Januari 8 mtaani Lavington kando ya barabara ya Gitanga, kaunti ndogo ya Dagoretti, kaunti ya Nairobi.

Karatasi ya mashtaka inasema mshtakiwa alimgusa JPN matako kwa mikono yake kinyume na kanuni za adhabu.

Kulingana na wapelelezi, mlalamishi alikuwa kwenye hoteli moja na mlinzi huyo ambaye alidai apewe chai.

Polisi wanasema kuwa mwanamke huyo ambaye anafanya kazi ya uhudumu  katika hoteli hiyo alimwambia mshtakiwa kuwa hakukuwa na maziwa lakini akasisitiza apate chai na kumlazimisha amwandalie chai nyeusi.

“Sikujua kamwe kwamba walinzi wengine wawili hawakuwa wameripoti kazini. Mpangaji pia alikuwa hajaripoti kazini. Nilikuwa kazini na mshtakiwa,” mlalamishi alisema kwenye ripoti ya polisi.

Taarifa ya polisi inaongeza kuwa baada ya mshitakiwa kunywa chai, aliondoka na kurudi baadaye akidai chai zaidi ambayo aliahidi kulipia.

Mwanamke huyo aliwaambia polisi kwamba mshtakiwa alianza kummiminia maneno ya sifa akisema ni mkarimu, mrembo na ana umbo zuri huku akianza kumshikashika matako kwa mikono yake.

Alisema hiyo ilikuwa mara ya pili kwa mshtakiwa huyo kumfanyia vitendo hivyo. Mshitakiwa huyo alikamatwa kwa kosa hilo baada ya mwathiriwa kuwasilisha malalamiko yake kwa polisi na kupelekea kuwasilishwa kwake mahakamani.

Mshtakiwa alikana kutenda kosa hilo mbele ya Hakimu mkuu wa Kibera Derrick Kuto na kuachiliwa kwa bondi ya Sh300, 000 . Hakimu aliagiza kwamba kesi hiyo itajwe baada ya wiki mbili.

Kuto pia aliagiza mshtakiwa apewe taarifa za shahidi na ushahidi wa maandishi ambao upande wa mashtaka utategemea kesi nzima.


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved