Wanafamilia wane walifikishwa mahakamani siku ya Jumatatu na kushtakiwa kwa mauaji baada ya viungo vya mwili wa mwanadada mmoja kudaiwa kupatikana ndani ya sufuria kubwa ya kupika supu.
Kulingana na ripoti kutoka vyombo vya kimataifa, mwanadada marehemu ambaye alikuwa ni mwanafasheni kwa jina Abby Choi kutoka Hong Kong aliuawa kwa njia tatanisha na kinyama mno huku mwili wake ukiwa umenyofolewa viungo tofauti ukipatikana.
Mume wa zamani wa Choi Alex Kwong, 28, kaka yake Anthony, 31, na baba yao, Kwong Kau, 65, wanashtakiwa kwa mauaji yake. Mamake Alex Kwong Jenny Li, 63, anashtakiwa kwa kupotosha njia ya haki, CNN walinukuu taarifa ya chombo cha habari kutoka Hong Kong.
Kulingana na CNN, Choi aliripotiwa kutoweka Jumatano wiki jana na msako dhidi yake ulipoanzishwa, Siku ya Jumapili, wachunguzi waligundua fuvu la kichwa, mbavu na nywele kadhaa, zinazoaminika kuwa mabaki ya Choi, kwenye sufuria kubwa ya chuma cha pua, polisi walisema. Sehemu nyingine za mwili, ikiwa ni pamoja na kiwiliwili cha Choi na mikono, bado hazipo.
Kikataji nyama, msumeno wa umeme, na baadhi ya nguo pia zilipatikana nyumbani, polisi walinukuliwa katika taarifa hiyo.
Taarifa zilisema kwamba mwanadada huyo Choi ambaye alikuwa mwanamitindo ni mtu maarufu sana Hong Kong na tayari ana ufuasi wa Zaidi ya watu laki moja.
“Hivi majuzi alionekana kama kielelezo cha jalada la kidijitali la jarida la kifahari la L'Officiel Monaco na alihudhuria Wiki ya Mitindo ya Paris ya mwaka huu,” CNN waliripoti.
Kesi hiyo iligubika jiji mwishoni mwa juma huku habari mbaya za uchunguzi zikitawala vichwa vya habari katika vyombo vya habari vya ndani na maelfu ya watu waliacha rambirambi kwenye akaunti za mitandao ya kijamii za Choi.
Mahakama iliahirisha kesi hiyo hadi Mei 8 ili kuruhusu uchunguzi zaidi wa polisi, shirika la habari la Hong Kong, RTHK waliripoti.
