Mbunge wa New Zealand amejiuzulu kutoka bungeni baada ya kuibuka kwa tuhuma nyingi za wizi wa dukani dhidi yake.
Kwa mujibu wa jarida la Independent, Kanda ya CCTV ziliibuliwa zikimuonyesha Mbunge huyo kwa jina Golriz Ghahraman akijaribu kuiba vitu kutoka kwa angalau maduka mawili ya nguo za hali ya juu huko Auckland na Wellington.
Katika maoni ya kwanza tangu madai hayo kuwasilishwa dhidi yake, Bi Ghahraman alinukuliwa na vyombo vya habari akisema:
"Ni wazi kwangu kwamba afya yangu ya akili inaathiriwa vibaya na mikazo inayohusiana na kazi yangu. Hii imenifanya nitende kwa njia zisizo za tabia kabisa. Sijaribu kusamehe matendo yangu, lakini nataka kuyaeleza.”
"Watu wanapaswa, kwa usahihi, kutarajia viwango vya juu zaidi vya tabia kutoka kwa wawakilishi wao waliochaguliwa. Nilipungukiwa. Samahani."
Aliongeza: "Jambo bora zaidi kwa afya yangu ya akili ni kujiuzulu kama mbunge na kuzingatia kupona kwangu na kutafuta njia zingine za kufanyia kazi mabadiliko chanya ulimwenguni."
Mnamo tarehe 10 Januari, Newstalk ZB Plus iliripoti kwa mara ya kwanza shutuma dhidi ya mbunge huyo mwenye umri wa miaka 43, ikidai alihusika katika wizi wa duka wakati wa msimu wa sikukuu katika Scotties Boutique, duka la bidhaa za kifahari katika kitongoji cha Auckland cha Ponsonby.
Polisi walikiri kulikuwa na uchunguzi juu ya madai hayo, lakini hawakuweza kuthibitisha utambulisho maalum wa mtu binafsi wakati huo.
