Mchungaji mmoja wa Kiafrika aliyetabiri kuwa naibu rais wa zamani wa Marekani Kamala Harris angeshinda uchaguzi wa urais na kuwa mwanamke wa kwanza kuwa rais katika taifa hilo, ameshindwa pa kuficha aibu yake baada ya Trump kuibuka mshindi.
Mchungaji maarufu wa Nigeria, Apostle Johnson Suleman
alirekodiwa miezi michache iliyopita akitabiri kuwa Mungu amempa maono na
ufunuo kwamba Marekani itapata rais wa kwanza mwanamke katika historia yao.
Hii ni baada ya chama cha Democrats kumkabidhi Harris
tikiti ya kumenyana na Trump wa Republican, baada ya rais Joe Biden
kushinikizwa hadi kujiondoa kwenye kinyang’anyiro hicho.
Mchungaji Suleiman kwa madaha, alisimama kwenye
mimbari takatifu na kuwadanganya wuamini kwamba Mungu amemnenea katika ndoto
kuwa Harris atamshinda Trump kwa kura nyingi ajabu.
Mtume Suleman, mwinjilisti wa televisheni na
mchungaji mkuu na mwangalizi mkuu wa Omega Fire Ministries International katika
video ya unabii alipokuwa akizungumza na waumini wake aliwathibitishia kuwa
Kamala Harris atashinda uchaguzi wa Marekani, akidai kuwa Mungu alisema naye.
Akiongea zaidi, Mtume Suleman anawaambia wasikilizaji
wake waandike kwani anaamini sana alichoambiwa na Mungu wake kuwa Makamu wa
Rais Kamala Haris atamshinda Donald Trump wakati wa uchaguzi.
Hata hivyo, mwisho wa siku, utabiri wa mtume Suleman
ulikosea kabisa huku rais wa zamani Donald Trump akishinda uchaguzi wa Marekani
dhidi ya Kamala Harris.
Mgombea wa chama cha Republican Donald Trump alipita
kwa raha kura 270 za uchaguzi zinazohitajika kushinda Ikulu ya White House, na
kupata kura 292, huku Mdemokrat Kamala Harris akipata 224.
Baada ya hali halisi kutimia, watu katika mitandao ya
kijamii wamemkabili vikali mchungaji huyo kujieleza ni wapi utabiri wake
ulikwenda fyongo.
Mchungaji huyo ametoweka mitandaoni bila kuzungumza chochote
kuhusu uchaguzi wa Marekani ambao ulifuatiliwa zaidi barani Afrika.