logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Pastor Ng’ang’a aonya waumini dhidi ya kufurahia kauli za ‘Anguka Nayo’ na ‘Mapangale’

“Wale ambao mtakuja kuwa wahubiri, mkuwe makini na kusema hii hamtaimba hapa kanisani, nendeni mkaimbe huko kwa baa. Hamtaimba hizo nyimbo hapa,” Ng’ang’a alisema.

image
na MOSES SAGWE

Burudani25 November 2024 - 09:48

Muhtasari




MCHUNGAJI wa kanisa la Neno Evangelism, James Maina Ng’ang’a ameonya waumini dhidi ya matumizi ya kauli tata ambazo zimeibukia mitaani.

Akizungumza katika moja ya ibada zake Jumapili iliyopita, Ng’ang’a alisema kwamba kauli hizo ambazo zinatumiwa na vijana wengi si za kufurahisha kwa macho na maskio ya waumini, akitoa onyo kali dhidi ya matumizi yake.

Mchungaji huyo alisema kwamba kauli kama ‘Anguka Nayo’ iliyoibuka miezi michache iliyopita na ile ya ‘Mapangale’ ambayo imewagawanya watumizi wa mitandao ya kijamii katika kipindi cha wiki moja iliyopita ni kauli potofu zisizo na nafasi hata kidogo katika maisha ya walio okoka.

“Hizi lugha zimetokea wewe uliyeokoka usizizungumze. Maana zimekuja lugha zenye zina ushetani. Hayo maneno wanaita sio hivyo, hizo nyimbo, sikiliza… kuna mmoja aliniambia eti anguka nayo. Hiyo ni yao. Alisema hiyo sijui na gani inaitwa ‘panga panga’ ni yao hiyo,” Ngang’a alisema.

Aliwashauri waumini wake na haswa wale ambao wanazimia kuja kuwa wahubiri kutochochewa na kauli kama hizo akisema kwamba ni heri wasizikubali kabisa katika mihadhara yao ya injili.

Mchungaji Ng’ang’a alisema kwamba kauli kama hizo ni za sajili ya kwenye vilabu vya starehe na wala si kwenye mikutano ya injili kama kanisani.

“Wale ambao mtakuja kuwa wahubiri, mkuwe makini na kusema hii hamtaimba hapa kanisani, nendeni mkaimbe huko kwa baa. Hamtaimba hizo nyimbo hapa,” Ng’ang’a alisema.

Mchungaji huyo alitoa kauli hiyo ikiwa ni wakati ambapo watumizi wa mitandao ya kijamii wamegawanyika katika matumizi ya kauli hizo mitaani.

Wiki iliyopita, mitandaoni kulikuwa na mjadala mkali kuhusu kauli ya ‘Mapangale’ ambayo ilibuniwa siku chache zilizopita.

Watu walikuwa wanajadili matumizi ya kauli hiyo ambayo iliasisiwa na mshereheshaji Zendiambo, wakisema kwamba ilikuwa inaunga mkono visa vya mauaji ya wanawake ambayo yamekithiri humu nchini.

Hata hivyo, Zendiambo alijitokeza na kutetea ‘mapangale’ dhidi ya madai hayo akisema kwamba ni kauli ya mtindo wa kucheza densi vilabuni tu.

Aidha, alisema kwamba hakuna aliyeshrutishwa kuitumia, akiwataka wale wanaohisi ni ya uchochezi kuiacha kwa matumizi ya wale wanaoielewa.

Mjadala kuhusu uhalali wa kauli hiyo unajiri wakati ambapo mauaji dhidi ya wanawake limekuwa ni kero humu nchini katika miezi ya hivi karibuni, baadhi ya watu wakiitaka serikali kutangaza mauaji dhidi ya wanawake kuwa janga la kitaifa.

Kwa upande mwingine, kauli ya ‘Anguka Nayo’ ilipata mwamko wa kipekee wakati wa maandamano ya vinana wa Gen Z dhidi ya mswada wa kifedha wa mwaka 2024.

Shinikizo la maandamano ya wiki kadhaa liliona rais Ruto akiufutilia mbali mswada huo, katika kile vijana walisema kwamba amelazimika ‘kuanguka’ na mswada huo.

Kauli hii iliwachochea vijana wanamuziki wa kundi la Wadagliz kuachia wimbo ‘Anguka Nayo’ ambao uliwavutia wengi na kuufanya kuwa kibwagizo cha kila sehemu.

Kilele cha umaarufu wa wimbo huo uliwapa vijana hao nafasi adimu ya kumtumbuizia rais na wageni wake katika uwanja wa Kwale wakati wa sherehe za kuadhimisha siku ya mashujaa mnamo Oktoba 20.



RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved