KWA mara ya kwanza baada ya kuachia video ya wimbo
wake mpya wa ‘Antennae’, msanii Zuchu amezungumzia ubunifu alioutumia kwenye
video ile.
Akizungumza na waandishi wa Habari za burudani katika
angatua ya JKIA baada ya kuwasili kwa ajili ya shoo yake nchini Kenya Jumamosi,
Zuchu aliulizwa kuhusu ubunifu huo ambao kwa wengi umeeleweka kuwa si wa
kawaida.
Baadhi ya watu ambao wameitazama video hiyo walihisi
kwamba ubunifu wa Zuchu kutokea akiwa na vazi lisolo la kawaida ambalo linatoa
picha ya kishirikina vile na alitakiwa kunyoosha maelezo kuhusu mtazamo huo.
Zuchu alikanusha uhusiano wowote na nguvu za giza
akisema kwamba wale wanaomjua kwa undani watamwambia mtu yeyote wakati wowote
kwamba huo ni uigizaji tu na hamna lingine zaidi.
“Kwa
wale wanaonijua watakuambia ile ni video tu. Mimi nampenda Mungu kuliko kitu
kingine chochote, hata sijui kama hicho kitu kinachoitwa ‘iluminati’ ni cha
kweli.”
“Ile
ilikuwa acting tu, nilitaka tu kuwa na kitu kipya kabisa wakati nafanya video
nikiimba, hivyo tu,” Mrembo huyo alijieleza kwa maelezo
ya kina.
Zuchu aliandamana na Diamond kwa ajili ya shoo ya
Furaha Fest ambayo ilifanyika Jumamosi jijini Nairobi.
Lakini Zuchu si wa kwanza kujikuta kwenye kikaango
cha mashabiki kutokana na muonekano kwenye video yake.
Mwaka jana, msanii wa Nigeria, Rema alizua mjadala
mkali mitandaoni baada ya kutoa picha na video zenye muonekano ambao
uliwakanganya mashabiki wake wengi.
Uvumi huo ulimlazimu Rema kunyoosha maelezo naye
akisema tu kwamba hamna dhana yoyote zaidi ya ubunifu tu.
Rema aliandika, “RAVAGE UPRISING/ Shaba za Wahenga
Wangu hukaa kwenye jumba la makumbusho la jiji hili hili, kwa hivyo
nilitengeneza yangu upya. Kwa hivyo, Edo amefafanuliwa upya, ramani imeundwa
upya, akili zako zimeamshwa na kinyago kuzaliwa upya. Asante London! 🦇🇬🇧”
Awali, shoo yake iliyotarajiwa kufanyika nchini
Ethiopia ilifutiliwa mbali kwa kile tetesi zilisema kuwa ni utata uliozunguka
mkufu wake wa shingoni.
Mkufu huo ulidaiwa kuwa na mchoro wa kanisa
linalochomeka lakini pia misalaba iliyopinduliwa juu-chini.