
MWANAMUME mmoja amezua mjadala katika mitandao wa TikTok baada ya video yake akisherehekea siku ya kuzaliwa ya mbwa wake kuenea.
Katika video hiyo, jamaa huyo alipamba
ukumbi wake kwa puto za rangi tofauti kumuenzi mbwa wake aliyekuwa anaongeza mwaka
mwingine katika maisha yake.
Jamaa huyo pia aliongeza mvuto katika
sherehe hiyo kwa kumchezea mbwa wake ala ya saxophone huku mbwa akichezesha
mkia kwa ishara ya furaha.
Alikuwa na marafiki na akamwalika mpiga
saxophonist kucheza muziki wa siku ya kuzaliwa kwa mbwa. Video hiyo mtandaoni
inanasa mshereheshaji akiwa amependeza na nyimbo kwenye hafla hiyo.
Video hiyo ilivutia maoni kinzani,
baadhi wakimpongeza kwa kumuenzi mnyama wake pendwa lakini pia wengine
walionekana kutofautiana naye kwa kile walihisi ni matumizi mabaya ya pesa.
Lakini je, suala la watu kusherehekea
siku za kuzaliwa kwa wanyama wao pendwa ni jambo geni?
Katika miaka ya hivi karibuni, watu
wamekuwa na hulka mpya ya kuwaonyesha upendo wa kiuhakika wanyama wao pendwa,
zaidi hata wanavyofanya kwa binadamu wenzao.
Mwaka 2022, mwanamume mmoja kutoka
nchini Kolombia aligonga vichwa vya habari alipoamua kuwaonyesha upendo mbwa
wake kwa kuwasherehekea na kuwaimbia nyimbo za heri njema za kuzaliwa.
Choko, ambaye anaishi mitaa ya
Bucaramanga nchini Colombia, hana mengi lakini alitumia alichokuwa nacho
kuwaandalia karamu ya siku ya kuzaliwa, kisha kurekodiwa na mpita njia.
Mnasa video huyo ambaye jina lake
halikutajwa alichukua video hiyo walipogundua mapenzi ambayo Choko alishiriki
na mbwa wake, Shaggy na Nena.
Walipogundua kwamba alikuwa amepatwa na
matatizo makubwa na keki na mishumaa, walimrekodi akiimba furaha ya kuzaliwa
kwa Shaggy na kumwonyesha upendo na uangalifu.