logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Kasisi wa Katoliki amkosoa pasta wa kanisa la kiroho kwa kudai Yesu hapendi maskini

“Madai ya kwamba “Yesu hakuwahi kumtembelea maskini yeyote katika nyumba yao” na kwa hiyo “Anachukia umaskini” si ya uwongo tu bali ni ya kupotosha kwa hatari.”

image
na MOSES SAGWEjournalist

Burudani18 April 2025 - 11:43

Muhtasari


  • Kasisi huyo wa Katoliki alitumia mifano kutoka vifungu mbalimbali vya Biblia kumpiga misururu wa makumbo pasta huyo akimkosoa kuhusu kueneza dhana ya Yesu kuchukia maskini.
  • “Madai ya kwamba “Yesu hakuwahi kumtembelea maskini yeyote katika nyumba yao” na kwa hiyo “Anachukia umaskini” si ya uwongo tu bali ni ya kupotosha kwa hatari.”

Kasisi wa Katoliki Chinaka Justin Mbaeri akosoa mahubiri wa mchungaji David Ibiyeomie //FACEBOOK

SIKU chache zilizopita, video ya mchungaji David Ibiyeomie wa Salvation Ministries nchini Nigeria akihubiri kwamba Yesu hapendi watu maskini na hakuwahi tembelea mtu maskini na kuingia katika nyumba yake ilizua mjadala pevu mitandaoni.

Watu mbali mbali wameichambua video hiyo na kutoa majibu yao, baadhi wakihisi kwamba mchungaji huyo alikuwa anawapotosha waumini wake kuhusu chuki ya Yesu kwa maskini.

Mmoja kati ya wakosoaji wa mahubiri hayo ni kasisi wa kanisa katoliki kutoka nchini Nigeria, Chinaka Justin Mbaeri ambaye anahisi pasta David Ibiyeomie alivuka mipaka katika kile anahisi ni kudanganya kondoo wa Bwana.

Kasisi huyo wa Katoliki alitumia mifano kutoka vifungu mbalimbali vya Biblia kumpiga misururu wa makumbo pasta huyo akimkosoa kuhusu kueneza dhana ya Yesu kuchukia maskini.

“Madai ya kwamba “Yesu hakuwahi kumtembelea maskini yeyote katika nyumba yao” na kwa hiyo “Anachukia umaskini” si ya uwongo tu bali ni ya kupotosha kwa hatari.”

“Inapotosha maisha ya Kristo na huduma yake thabiti kwa maskini. Utume wa Yesu, kama ulivyofunuliwa katika Maandiko na kuthibitishwa na Kanisa, ulielekezwa haswa kwa maskini, waliotengwa, na wa hali ya chini (rej. Luka 4:18) - "Roho wa Bwana yu juu yangu ... amenitia mafuta kuwahubiri maskini Habari Njema." Hakuwavumilia tu maskini, aliwatanguliza - chaguo la upendeleo kwa maskini (rej. Mathayo 11:5)” kasisi alieleza.

Alinukuu kifungo kingine cha kueleza kwamba Yesu alizaliwa katika familia ya umaskini na hivyo haileti maana kuzua dhana kwamba hapendi watu maskini wakati wazazi wake walikuwa watu wa maisha ya kawaida tu.

“Yesu alizaliwa katika umaskini, amevikwa nguo za kitoto, na kulazwa horini (Luka 2:7). Alikula pamoja na watoza ushuru na wenye dhambi, naam, lakini pia na wakulima wanyenyekevu, wavuvi, na watu waliotengwa. Hakuchagua mali wala maisha ya ikulu. Je, tuseme Alijichukia Mwenyewe?” Kasisi Mbaeri alihoji.

Kasisi huyo alikosoa Kauli ya pasta kwamba Lazaro hawakuwa maskini na ndio maana Yesu alipowatembelea nyumbani kwao walimpa chakula, akisisitiza kwamba Biblia yenyewe inawatambulisha kama maskini.

“Kudai kwamba Yesu alimtembelea Lazaro wa Bethania, ndugu ya Mariamu na Martha, na kwamba walikuwa wakimpa chakula, haimaanishi kwamba walikuwa matajiri. Hii inafichua upuuzi wa Mchungaji Ibiyeomie wa maana ya mji wa nyumbani wa Lazaro, ambao ni Bethania. Bethania kwa Kiebrania ni "Beth anya" (בֵּית עַנְיָה), ambayo ina maana ya "Nyumba ya Maskini" au "Nyumba ya Mateso."

Katika video hiyo ya kama dakika moja hivi, mchungaji David Ibiyeomie alidai kwa ukakamavu kwamba Yesu hapendi maskini ndio maana hakuwatembelea katika miaka yake 33 ya huduma duniani.

"Yesu hakuwahi kumtembelea maskini yeyote katika Biblia. Chunguza Biblia yako. Yesu hakuwahi kuingia katika nyumba ya mtu maskini. Hiyo ina maana anachukia umaskini. Angalia, alimtembelea Lazaro, hawakuwa maskini walikuwa wakimpa chakula. Alimtembelea Mwenye dhambi aitwaye Zakayo, ambaye alikuwa tajiri. Niambie maskini mmoja Yesu aliingia nyumbani kwake? Anachukia umaskini, hiyo ndiyo maana - Anachukia watu ambao sio maskini…”

Kama ulikosa video hiyo, itazame kwenye chapisho letu la awali hapa:

 

Makala Zinazohusiana


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved