Mbunge wa Homa Bay, George Peter Kaluma, amedai kuwa katika utamaduni wa Wajaluo, hakuna anayeweza kuchaguliwa kuwa kiongozi ikiwa hajaoa.
Alifafanua kuwa kiongozi ni lazima awe na chakula na mke wa kupikia jamii, akibainisha kuwa wananchi hutegemea kuwe na mtu nyumbani wa kuwapokea na kuwalisha wanapomtembelea kiongozi wao.
“Kwenye nchi ya Waluo huwezi kuchaguliwa kama hujaoa. Ni nani atakayewalisha watu? Kwa Waluo, kiongozi ni lazima awe na chakula na awe na mke wa kupikia watu,” Kaluma alisema.
“Kwa Waluo, mke anatarajiwa kuilisha jamii. Tofauti na jamii nyingine, katika jamii ya Waluo huwezi kuchaguliwa kwa jambo lolote ikiwa hujaoa. Ni lazima uwe umeoa," aliongeza.
Alisisitiza kuwa kiongozi aliye na mpangilio nyumbani huwa pia na mpangilio kazini.
“Tunaweza kukuonea huruma ukiwa mjane, lakini mwanzoni ni lazima uwe umeoa kwa sababu watu wanapokuja nyumbani wanataka mtu wa kuwapikia, wanataka mtu wa kuwapokea, wa kuwakaribisha, na ukiwa na mpangilio nyumbani, inamaanisha unaweza pia kuwa na mpangilio ofisini,” aliongeza.
Mbunge alisisitiza kuwa, tofauti na jamii nyingine nchini, katika jamii ya Waluo, wapigakura hutafuta viongozi waliooa na wanaoishi kwa mpangilio nyumbani, akieleza kuwa mtu asiye na mwenza hupata ugumu kuhusiana na wananchi wanaotafuta mapokezi na uangalizi wa kifamilia.
Kaluma aliongeza kuwa ingawa wanaume waliopoteza wake wanaweza kuangaliwa kwa huruma, mgombea ni lazima awe ameoa tangu mwanzo.