Utafiti uliofanywa na mashirika mengi tu unaonesha wanaume wanapenda mchezo wa kandanda kwa asilimia kubwa kuliko wanawake ambao kwa upande wao wanapenda filamu aina ya Soap Operas.
Mapenzi ya mchezo wa kandanda kwa wanaume yamepelekea mpaka wengine wanafanyiana utani kuhusu ubabe wa timu wanazozipigia upato huku wengine wakizamia katika masuala ya ubashiri na uchezaji wa kamari kupitia michezo ya soka.
Wiki hii pamesambazwa mitandaoni video moja inayomuonesha mwanaume mmoja ambaye mpaka sasa hajatambulika akiwa anashabikia timu yake uwanjani kwa mbwembwe za ajabu huku akichezesha mwili kwenye kiti.
Video hii ambayo ilianzia kwenye mtandao wa Twitter inamuonesha bwana huyo akiwa amejisahau kabisa kwamba anarekodiwa huku macho yake na fikira zote amezitundika uwanjani, mwili ndio unacheza kwenye kiti kama mchezaji wa kumi na mbili uwanjani.
Baadhi ya waliotolea maoni yao kwenye video hiyo walisema huu ndio ushabiki wa kweli na mapenzi kwa soka huku wengine wakisema bwana huyu huenda alikuwa amewekeza na ndio maana hakuwa anatulia kwenye kiti wakati alikuwa anaona kama timu yake inakaribia kutikiza wavu wa timu pinzani.
“Anawachenga kama ameketi down, akapeana pass striker akashindwa kufunga,” mmoja aliachia maoni yake.