Madaktari wa Katoliki wanataka kuondolewa kabisa kwa muswada wa afya ya uzazi, 2019, wakisema kwamba unakinzana na katiba na maadili ya kitaifa na yale wa Kikristo.
Muungano wa madaktari wa katoliki nchini (KCDA) ulisema kwamba muswada huo una tofauti kidogo mno na ule uliyokuwa unapendekezwa na seneta Judy Sinjeny wa mwaka 2014.
Soma habari zaidi;
Muungano huo ulisema kwamba muswada huo mpya unapendekeza watoto wa chini ya miaka 18 kupata dawa za kupanga uzazi na huduma za kuavya mimba, huku mabadiliko ya pekee yakiwa kwamba lazima wapate idhini ya wazazi wao.
“Tuna wasilisha kwamba muswada huo hauna nafasi katika Jamhuri ya Kenya na unafaa kuondolewa kutoka orodha ya miswada iliyo katika seneti,” Muungano huo ulisema wakati ukiwasilisha maoni yake kwa kamati ya afya ya seneti.
Muswada huo unaopendekezwa na seneta wa Nakuru Susan Kihika pia ulipingwa na viongozi wa Kiislamu na wenzao wa dini Kikristo. Hata hivyo mashirika mawili ya serikali yanaunga mkono muswada huo.
Soma habari zaidi;
Tume ya kitaifa ya haki za binadamu (KNCHR) na baraza la kitaifa la idadi ya watu na maendeleo (NCPD) yalipongeza muswada huo yakisema kwamba unalenga kutambua umuhimu wa haki ya afya ya uzazi kwa kila mtu.
Shirika la KNCHR lilisema kwamba muswada huo unawiana na katiba, inayosema kwamba kila mtu ana haki ya kupata huduma bora za afya.
Madaktari wa katoliki kwa upande wao walidai kwamba kufunza jamii kuwa starehe ya ngono ni haki kutapelekea kuwepo kwa waraibu wa ngono.
