Mwanamke mwenye umri wa miaka 30 anayedai kupigwa na mbunge wa Nakuru West Samuel Arama katika eneo la Kaptembwa analilia haki.
Amanda Chesiyna, ambaye ni mkulima katika eneo la Molo, anadai kuwa mbunge huyo alimshambulia alipokuwa ameenda kudai lori ambalo lilimilikiwa na marehemu babake Elisha Chebii-aliyekuwa naibu kamishna wa ardhi.
Chesiyna alisema kwamba mbunge huyo alimpiga kofi na teke hadi akaanguka, kabla ya wasaidizi wa mbunge huyo kumvamia na kumshambulia pia huku maafisa wa polisi wakitazama.
Video ambayo imechipuka inaonyesha mwanamke mmoja akikabiliana na mbunge huku mbunge huyo akimuonya dhidi ya kuendelea kumzomea na kumkaripia.
Arama kisha anamuambia mwanamke huyo kwamba atampiga naye akamdhubutu kufanya hivyo. Mbunge huyo kisha anaonekana akimsongea na kumpiga. Anaanguka chini na anasikika akilia.
Alipoulizwa na meza ya habari ya ‘The Star’, mbunge huyo hakukana madai ya Chesiyna “Andikeni mnachotaka,” alisema.
Chesiyna alisema kwamba familia yake ilikuwa katika harakati za kuchukuwa mali iliyokuwa imeachwa na marehemu baba yao, aliyefariki mwezi Mei mwaka huu.
“Mali yetu ilikuwa inapotea baada ya kifo cha babangu, lakini tulikuwa tunaona mali kama vile magari yakizunguka mjini Nakuru,” alisema.
Alisema kwamba familia ya marehemu babake ilikwenda mahakamani kutafuta idhini kusimamia mali ya babake ombi ambalo walipewa na mahakama ya Milimani, Nairobi.
Alisema lori hilo lilikuwa likiendelea kubeba mchanga mjini Nakuru, na hawakujua nani alikuwa ametwaa umiliki wa lori hilo.
Baada ya kushambuliwa, Chesiyna alisema kwamba alikwenda katika kituo cha polisi cha Kaptembwa na kupata jamaa aliyekuwa amepiga (Arama) tayari amefika katika kituo hicho cha polisi.
Alitibiwa katika hospital ya Anidad Medical Clinic.
Aliandikisha taarifa kwa polisi chini ya nambari ya OB 15 , 30/11/2020
