logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Sitaki kupendekezwa na rais Uhuru ama mtu yeyote- Raila

Raila alisema kuwa iwapo ataamua kugombea urais hatatafuta pendekezo la rais ila atakachotaka ni kura yake tu.

image
na Radio Jambo

Habari08 July 2021 - 07:41

Muhtasari


•Akiwa kwenye mahojiano katika stesheni moja ya redio nchini,  Raila amesema kuwa hajawahi kutegemea yeyote kumpendekeza anapowania kiti chochote.

•Raila pia alieleza imani yake kuwa BBI itarejea huku akisema kuwa bado kuna nafasi ya kura ya maoni kufanyika ili kurekebisha katiba kabla ya uchaguzi mkuu.

Raila Odinga

Kinara wa ODM Raila Odinga amepuuzilia mbali madai kuwa anataka rais Uhuru Kenyatta ampendekeze kama mridhi mwafaka wa kiti atakachokipungia buriani mwaka ujao.

Akiwa kwenye mahojiano katika stesheni moja ya redio nchini,  Raila amesema kuwa hajawahi kutegemea yeyote kumpendekeza anapowania kiti chochote.

"Sijasema na hata Uhuru mwenyewe hajasema atapendekeza mtu. Mimi sitaki kupendekezwa na Uhuru ama mtu yeyote.Uhuru si unajua tulishindana na yeye, atanipendekeza namna gani?" Raila alisema.

Raila alisema kuwa ushirikiano wake na rais ni wa kikazi tu ila sio wa kisiasa. Alisema kuwa alikubali kumsaidia Uhuru kutekeleza ahadi zake kwa Wakenya.

"Yeye tumekuwa naye na tukaongea mambo mengi kirefu. Alinieleza shida ambazo alipata kipindi kile cha kwanza . Akasema kuwa sasa anataka kuleta mabadiliko ili aweze kutimiza ile ahadi ambayo alipatia Wakenya kisha aende nyumbani na nikasema ni sawa mimi naheshimu hayo" Raila aliendelea kusema.

Ingawa alisita kuzungumzia mipango yake ya kisiasa akisema kuwa atazungumza baada ya kura  ya maoni, Raila alisema kuwa iwapo ataamua kugombea urais hatatafuta pendekezo la rais ila atakachotaka ni kura yake tu.

"Sitaki kupendekezwa na Uhuru. Ile mimi nitataka ni kura  yake" Raila alisema.

Raila pia alieleza imani yake kuwa BBI itarejea huku akisema kuwa bado kuna nafasi ya kura ya maoni kufanyika ili kurekebisha katiba kabla ya uchaguzi mkuu.


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved