Klabu za Primia Ligi zitakutana Jumatatu kujadili mzozo unaoendelea unaozingira janga la virusi vya corona.
Huku mechi tisa zikiahirishwa katika kipindi cha wiki moja iliyopita, ikiwa ni pamoja mechi tano za wikendi hii mechi zilizokuwa kwenye ratiba, klabu zinataka muda wa kujadili nini la kufanya.
Mameneja na manahodha pia watafanya mikutano yao.
Meneja wa Aston Villa Steven Gerrard alisema kuwa anamatumaini mkutano huo utaweka "mambo wazi " kuhusiana na "hofu kubwa zilizopo na maswali ambayo hayajajibiwa''.
Wakati huo huo, Mkuu wa Primia Ligi Richard Masters ameziandikia klabu akitaka wachezaji wote wachanjwe na kusisitiza umuhimu wa kumalizika kwa msimu wa Ligi.
Nae meneja wa Brentford Thomas Frank alikuwa wa kwanza kutoa wito wa kusitishwa kwa mechi zote hadi tarehe 26 Disemba ili kuwezesha kupangwa kwa mpango mpya.
Baadhi wanahisi mapumziko yanapaswa kuwa marefu zaidi -lakini wengine kama Meneja wa Liverpool Jurgen Klopp hawaamini hilo linapaswa kufanyika.
Primia Ligi ilisema Alhamisi kwamba inalengo la kuendelea kucheza mechi ili mradi ni salama kufanya hivyo.
Wakati huo huo, meneja wa , Manchester City Pep Guardiola ameruhusiwa kufufua maandalizi kwa ajili ya safari ya kuelekea Newcastle.
Muhispania huyo alilirejesha kipimo cha virusi vya corona ambacho hakikuwa kimekamilika na kuahirisha mkutano wa Ijumaa aliopanga kuufanya na waandishi wa habari, lakini kipimo cha haraka cha Covid PCR kiliporudi matokeo yalikuwa ni hasi.
'Tunahitaji mambo yawe wazi' - Klabu zilisema nini Ijumaa?
Meneja wa Arsenal Mikel Arteta: "Masharti yatatoa uamuzi juu ya iwapo mechi inachezwa au hapana, lakini tunahitaji kuelewa sababu nyuma ya uamuzi
"Tutalazimika kutafuta njia. Tulifahamu wakati tulipoanza msimu huu matatizo ya Covid, kuwa hili huenda likatokea na nina uhakika kulikuwa na mpango A, B na C. Tunahitaji mambo yawe wazi."
Meneja wa Aston Villa s Steven Gerrard: "Sote tunataka kitu saw ana tunataka mechi ziendelee. Sina hofu lakini nina Imani katika Primia Ligi na watu wanaochukua maamuzi.
"Kuhusu kuwa katika nafasi yangu ninapaswa kuandaa timu vyema niwezavyo. Tumekuwa na visa katika baadhi ya wachezaji na tumekuwa na baadhi ya visa vya maambukizi miongoni mwa wafanyakazi.
Meneja wa Liverpool Jurgen Klopp: "Sipingi kusimamishwa kwa ligi lakini sioni faida yake kwa 100% .
"Kusimamicha Ligi kunamaanisha kusimamisha sasa kwa wiki moja au wiki mbili, kwa hiyo ni kama mechi tano au sita. Ni lini unataka kuzicheza?
"Au tuendelee kucheza tu.Ni vigumu sana kwasababu kwa hatua kwa hatua wachezaji watapata maambukizi."
Meneja wa Chelsea Thomas Tuchel: " Haiko mikononi mwangu lakini lazima mambo yaeleweke na kuwa na uwazi kila mara katika kila jambo.
Pia kuna hofu miongoni mwa klabu ya kuwaachilia wachezaji kwa ajili ya kushiriki Kombe la mataifa ya Afrika mwezi ujao pamoja na michuano ya waliofuzu kwa kombe la dunia.
Je hali ikojeUlaya kuhusiana na corona?
Kufikia sasa Uingereza ndio nchi iliyoathiriwa zaidi miongoni mwa mataifa ya Ulaya, huku karibu watu 15, 000 wakithibitshwa kupata maambukizi ya kirusi kipya cha Omicron Ijumaa.
Katika maeneo yote ya bara hilo, maafisa wa afya wanakabiliana na wimbi la maambukizi.
Masharti zaidi ya kuzuwia kusambaa kwa virusi hivyo yalitangazwa na Ujerumani, Jamuhuri ya Ireland na Uholanzi Ijumaa huku serikali zikitaka kumaliza maambukizi,.
Ulaya tayari imeshuhudia visa zaidi ya milioni 89 na vifo vya watu milioni 1.5 vinavyohusiana na Covid, kulingana na takwimu za hivi karibu za EU.
Lakini waziri wa afya wa Ujerumani Karl Lauterbach aliwaambia waandishi wa habari Ijumaa kuwa nchi "lazima ijiandae kwa changamoto ambayo hatujawahi kuwa nayo kwa muundo huu", huku shirika lake la afya ya umma ikizitaja Ufaransa, Norway, na Denmark kama ''maeneo hatari'' kutokana na kuogezeka kwa maambukizi katika nchi hizo.
Ujerumani yenyewe iliripoti zaidi ya visa 42,000 vya maambukizi Jumamosi, vikiwa ni chini ya visa vipya 50,000 vya maambukizi vilivyorekodiwa Ijumaa.
Ireland, ambako theluthi ya visa vipya vimetokana na omicron, Taoiseach Micheál Martin alisema kuwa wanatarajia "kushuhudia maambukizi kwa kiwango ambacho ni zaidi ya kile ambacho kimewahi kushuhudiwa hadi sasa".
Tahadhari hiyo inakuja huku Uingereza ikiripoti idadi ya maambukizi kwa siku ya tatu- hadi watu 93,000- wengi wao wakiwa na maambukizi ya kirusi kipya cha Omicron.
Ufaransa ilifunga mipaka yake kwa watu wanaosafiri kutoka Uingereza kwa shuguli za biashara na utalii saa tano usiku Ijumaa, huku misururu mirefu ya watu ikishuhudiwa katika maeneo ya kuabiri ndege ya Port of Dover na Eurostar huku watu wakijarubu kuingia kabla ya marufuku ya safari kuanza kutekelezwa.
Mapema wiki hii , Italia, Ugiriki na Ureno zilitangaza kuwa wageni wote kutoka Muungano wa EU watahitaji kuwasilisha matokeo hasi ya covid wanapowasili-hata wale ambao wamechanjwa.