Ni rasmi sasa kwamba lugha ya Kiswahili imehalalishwa kuwa lugha rasmi kakita sehemu za kikazi barani Afrika.
Hii inafuatia ombi lililowasilishwa katika muungano wa mataifa ya Afrika, AU na naibu rais wa jamhuri ya Tanzania, Philip Mpango kutaka lugha hiyo itambulike rasmi katika sehemu za kazi.
Katika kutetea ombi hilo, Mpango alisema kwamba lugha ya Kiswahili ina watumiaji zaidi ya milioni 100 wanaoifanya lugha hiyo kuwa miongoni mwa lugha zenye wazungumzaji wengi zaidi barani Afrika.
Mpango alikitetea Kiswahili kwa kusema kwamba lugha hiyo imesambaa katika jamii nyingi katika muungano wa Afrika mashariki EAC, muungano na kimaendeleo wa mataifa ya kusini SADC, na vile vile ni lugha ambayo inafunzwa katika mataifa mengi ndani na nje ya Afrika.
Tangazo la kurasmisha lugha ya kiswahili lilitolewa katika bunge la wakuu wa mataifa ya bara Afrika mjini Addis Ababa, Ethiopia.
Itakumbukwa hii si mara ya kwanza kwa wajumbe wengi wa muungano wa AU kusukuma kurasmishwa kwa lugha ya kiswahili na ambapo shirika la UNESCO lilitangaza Julai 7 ya kila mwaka kuwa siku kuu ya Kiswahili duniani.
Kulingana na utafiti wa UN, lugha hiyo ina mizizi yake Afrika Mashariki na uzungumzaji wake umesambaa kwa takribani mataifa 14 yakiwemo Tanzania, Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Sudan Kusini, Somalia, Mozambique, Malawi, Zambia, Comoros, na mpaka Oman na Yemen katika mashariki ya kati.
Lugha hii ya kiswahili imezidi kukita mizizi huku mataifa kutoka kusini mwa Afrika kama vile Botswana na Jamhuri ya Afrika Kusini wakiwa wameyajumuisha katika mtaala wa masomo huku taifa la Namibia likitarajiwa kujiunga nao.
