logo

NOW ON AIR

Listen in Live

CJ Martha Koome anaunda benchi la majaji 3 kusikiliza ombi la Sonko dhidi ya chama cha Wiper

Chifu huyo wa zamani wa kaunti anatafuta maagizo ya kuzuiwa chama cha Wiper Democratic

image
na Radio Jambo

Habari30 June 2022 - 05:32

Muhtasari


•Anatafuta maagizo ya kuzuia tume hiyo kutochapisha karatasi za kupigia kura za wadhifa wa ugavana wa Mombasa katika uchaguzi mkuu ujao wa Agosti 9.

•Jaji Mkuu Martha Koome ameunda benchi ya majaji watatu kusikiliza na kuamua ombi la aliyekuwa gavana wa Nairobi Mike Sonko.


Aliyekuwa gavana wa Nairobi Mike Sonko

Jaji Mkuu Martha Koome ameunda benchi ya majaji watatu kusikiliza na kuamua ombi la aliyekuwa gavana wa Nairobi Mike Sonko.

Chifu huyo wa zamani wa kaunti anatafuta maagizo ya kuzuiwa chama cha Wiper Democratic kumteua mgombeaji  mwingine  kuchukua  nafasi yake katika kinyang'anyiro cha ugavana Mombasa.

Katika barua iliyoandikwa Juni 29 iliyotiwa saini kwa niaba yake na afisi ya mawakili mkuu wa jaji mkuu, Koome alidhibitisha  kuwa ameteuwa majaji watatu kusikiliza na kuamua suala hilo mjini Mombasa.

"Asante kwa barua yako ya Juni 27 mwaka huu iliyotumwa kwa mheshimiwa Jaji Mkuu. Nina maagizo ya kukujulisha kwamba CJ amepokea faili ya awali ya mahakama kutoka mahakama kuu ya Mombasa", sehemu ya barua hiyo ilidokeza.

Mnamo Ijumaa wiki jana, jaji wa Mahakama Kuu ya Mombasa Olga Sewe katika uamuzi wake, aliamuru kesi hiyo ipelekwe mbele ya Jaji Mkuu ili kumwezesha kuunda benchi ya kusikiza na kuamua kesi hiyo kwani inazua maswali makubwa ya sheria.

Katika kesi hiyo iliyowasilishwa katika mahakama kuu ya Mombasa, Sonko alidai kuwa  huenda akapata hasara kubwa ikizingatiwa kiasi cha pesa na muda aliowekeza katika azma yake ya kuwania kiti cha Ugavana.

Hasara hiyo anadai itatokana na kuisha kwa saa 72 zilizoruhusiwa na IEBC kwa chama hicho kusimamisha mgombeaji mpya kwa nafasi yake.

Anatafuta maagizo ya kuzuia tume hiyo kutochapisha karatasi za kupigia kura za wadhifa wa ugavana wa Mombasa katika uchaguzi mkuu ujao wa Agosti 9.


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved