Serikali ya Uchina imevunja ukimya wake kuhusu mzozo unaozingira China Square ikisema inatumai kuwa mzozo huo utasuluhishwa hivi karibuni.
Katika taarifa yake Jumatano, Ubalozi wa China nchini Kenya ulisema unaunga mkono kikamilifu uhusiano wa kibiashara kati ya China na Kenya na raia wake wanaofanya biashara nchini humo kwa kufuata sheria za Kenya.
“Wakati huo huo, tunatumai kuwa serikali ya Kenya italinda haki na maslahi halali ya makampuni ya China na raia wa China na kuweka mazingira ya biashara jumuishi na ya kirafiki ili kukuza ushirikiano wa vitendo kati ya China na Kenya na kuleta manufaa kwa nchi zetu mbili. na mataifa mawili,” ilisema taarifa hiyo.
Duka hilo kubwa la reja reja lilifunga shughuli zake kwa muda usiojulikana Jumapili ili kushughulikia maswala kadhaa ikiwa ni pamoja na usalama.
"Sisi, China Square Limited, tunasikitika kuwajulisha kuwa tutaendelea kufunga kwa taarifa zaidi," chombo hicho kilisema katika taarifa yake.
Mmiliki Lei Cheng almaarufu Charlie alisema kuwa atazingatia kuongeza wafanyikazi wa usalama ili kushughulikia msongamano mkubwa wa wateja na kuongeza idadi ya till kwenye duka kuu ili kurahisisha harakati za wateja.
"Tunahitaji kufunga na kutoa muda wa kupoa," alisema.
Siku ya Jumanne, wamiliki wa biashara katika CBD walifanya maandamano kulaani duka hilo kwa kile walichokiita mazoea ya biashara yasiyo ya haki.
Jumuiya ya wafanyabiashara walisema walikuwa wakipoteza wateja wa duka la Wachina lililoko Unicity Mall kwenye barabara ya Thika kutokana na bidhaa zake za bei ya chini.
Wafanyibiashara hao kutoka kitovu cha biashara cha Nyamakima walifanya maandamano kutoka katikati mwa jiji hadi Harambee Annex ambayo ina afisi ya Naibu Rais Rigathi Gachagua ili kutafuta mkutano naye.
Walipeperusha mabango yaliyoandikwa "Komesha uvamizi wa China, linda biashara zetu. Okoa kizazi chetu cha baadaye."