logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Jenerali Francis Ogolla ateuliwa mkuu mpya wa majeshi ya Kenya

Ogolla amechukua wadhifa huo kutoka kwa Jenerali Robert Kibochi ambaye anaondoka.

image
na Radio Jambo

Yanayojiri28 April 2023 - 12:44

Muhtasari


• Alipanda ngazi hadi kuwa Meja Jenerali na aliteuliwa kuwa Kamanda wa Jeshi la Wanahewa la Kenya Julai 15, 2018, wadhifa ambao amehudumu kwa miaka mitatu.

Jenerali Francis Ogolla ameteuliwa kuwa Mkuu mpya wa Majeshi ya Ulinzi katika mabadiliko katika jeshi.

Ogolla amechukua wadhifa huo kutoka kwa Jenerali Robert Kibochi ambaye anaondoka baada ya kutimiza umri wa lazima wa kustaafu miaka 62.

Rais William Ruto ambaye ni Amiri Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi siku ya Ijumaa alimpandisha cheo Ogolla hadi cheo cha Jenerali.

Kabla ya uteuzi huu, Jenerali Ogolla alikuwa Makamu Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi.

Ruto pia alimteua Luteni Jenerali Jonah Mwangi kuwa Makamu Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi (VCDF).

Kabla ya uteuzi huu, Luteni Jenerali Mwangi alikuwa Naibu Chansela, Chuo Kikuu cha Ulinzi cha Kitaifa - Kenya.

 

Meja Jenerali Said Farah anachukua nafasi kutoka kwa Luteni Jenerali Jonah Mwangi kama Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Ulinzi cha Kitaifa - Kenya.

 

Zaidi ya hayo, kwa ushauri wa Baraza la Ulinzi, linaloongozwa na Waziri wa Ulinzi Adan Duale ambalo lilikutana leo, Rais alikubali mapendekezo ya Baraza la Ulinzi na kutoa vyeo mbalimbali, vyeo na uteuzi katika idara ya jeshi.

 

Jenerali Ogolla ni mhitimu wa ÉcoleMilitaire de Paris na Chuo cha Kitaifa cha Ulinzi cha Kenya.

Ana Diploma katika Masomo ya Kimataifa na Sayansi ya Kijeshi kutoka Chuo Kikuu cha Egerton, Shahada katika Sayansi ya Siasa, Migogoro ya Silaha na Mafunzo ya Amani na Shahada ya Uzamili katika Mafunzo ya Kimataifa kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi.

 

Alipanda ngazi hadi kuwa Meja Jenerali na aliteuliwa kuwa Kamanda wa Jeshi la Wanahewa la Kenya Julai 15, 2018, wadhifa ambao amehudumu kwa miaka mitatu.

 

Meja Jenerali David Kimaiyo Tarus aliteuliwa kuwa naibu kamanda wa Jeshi la la nchi kavu huku Meja Jenerali William Shume akiteuliwa mkuu wa kitengo cha kulinda mipaka.

 

Meja Jenerali Alphaxard Kiugu aliteuliwa kuwa kamanda wa kikosi cha Jumuiya ya Afrika Mashariki-DRC kuchukua nafasi ya Meja Jenerali Jeff Nyagah ambaye aliteuliwa kuwa Mkuu wa kikosi cha Magharibi huku Meja Jenerali Eric Kinuthia akiteuliwa mkurugenzi mkuu wa Chuo cha Taifa cha Ulinzi cha wanahewa.

 

Aliyekuwa Mkurugenzi wa Ujasusi wa Kijeshi Meja Jenerali Said Mohamed Farah alihamishwa hadi Chuo cha Kitaifa cha Ulinzi na kuteuliwa Makamu wa Chansela huku Brig Yahya Abdi akiteuliwa kuwa naibu kamanda wa Jeshi la Wanamaji la Kenya.

 

Baraza hilo pia lilimpandisha cheo Brig John Nkoimo na kuwa Meja Jenerali na kumtaja kuwa Kamanda wa Chuo cha Uongozi wa Pamoja na Brig Abdulkadir Burje kuwa Meja Jenerali na kumtaja kuwa Mkurugenzi wa Ujasusi wa Kijeshi.

 

Brig Paul Owuor Otieno alipandishwa cheo hadi Meja Jenerali na kuteuliwa Mkurugenzi Mkuu wa Kenya Shipyards Limited huku Kanali Anthony Rotich akipandishwa cheo hadi Brig na kumtaja kamanda wa Kikosi cha Ujasusi cha Kijeshi.

 

Kanali Alfred Gitonga alipandishwa cheo na kuwa Brig na kuteuliwa kuwa mkurugenzi wa kituo cha uratibu wa kijeshi.

 

Maarufu Zaidi

RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2026. All rights reserved