Muungano wa Kenya Kwanza umetaja wanachama wake watano ambao watauwakilisha katika mazungumzo mapya yaliyopendekezwa na upande wa Upinzani.
Kikosi cha Kenya kwanza kitaongozwa na kiongozi wa wengi katika bunge la kitaifa Kimani Ichung'wah, na wanachama wengine wakiwa Aaron Cheruiyot (Kiongozi wa Wengi katika Seneti), Gavana wa Embu Cecile Mbaririe, Hassan Omar (Mbunge wa EALA) na mwakilishi wa kike wa Bungoma Catherine Wambilinga.
Kikosi cha Kenya Kwanza kinatarajiwa kuungana na wenzao wa Azimio wakiongozwa na kinara wa Wiper Kalonzo Musyoka pamoja na kiongozi wa Wachache Opiyo Wandayi, Eugene Wamalwa ambaye ni kinara wa DAP, Okong'o Omogeni na Mbunge wa Malindi Amina Mnyanzi. Kenya Kwanza katika taarifa siku ya Jumatano ilisisitiza kuwa watajadiliana na wenzao wa Azimio kuhusu masuala matano.
Maswala waliotajwa ni pamoja na kuundwa upya kwa tume ya IEBC; utekelezaji wa kanuni ya kijinsia ya theluthi mbili, uboreshaji wa hazina ya maendeleo ya maeneo bunge, kubuniwa kwa Ofisi ya Kiongozi wa Upinzani na Ofisi ya Mkuu wa Mawaziri.
Katika taarifa yake Kenya Kwanza ilisisitiza kuwa ghasia hazitakuwa tena na hazitakuwa sehemu ya mazungumzo ya kisiasa ya Kenya.
