Ajuza wa miaka 60 kutoka nchi jirani ya Tanzania aliyegonga vichwa vya habari wiki kadhaa zilizopita baada ya kukiri kuwa katika uhusiano wa kimapenzi na kijana wa miaka 27 amerejea tena ila safari hii kwa majonzi mazito baada ya kumfumania kijana huyo.
Ajuza huyo katika mahojiano ya moja kwa moja katika runinga ya Global TV Online nchini humo, alishindwa kuzuia mifereji ya machozi yake akielezea jinsi alivyomfumania kijana huyo akiwa na mwanadada mwingine.
Kwa mujibu wa ajuza huyo kwa jina Warda, alisema kwamba wamekuwa kwenye mapenzi na kijana huyo kwa muda wa miaka 3.
Wiki moja iliyopita alimfumania baada ya kuona picha na video zake mitandaoni akiwa kitandani na mwanamke ambaye aliweza kumtambua kwamba waliwahi kuzaa naye.
Alipomuuliza kijana wa watu alikula yamini kwa kukataa kabisa na Warda akamuambia kila mtu aende zake.
Cha kushangaza bibi huyo alisema kuwa tayari alikuwa ameshamnunulia gari lakini alimuacha akae nalo na wala hakutaka ngonjera zake.
“Nilimfuania, niliona picha. Natumia mitandao ya kijamii yote na nilimuona akiwa na msichana aliokuwa anakataa kwamba hajazaa naye. Nimeziona picha zao wako wote wamelala kitandani, na yeye alikataa katakata kusema kwamba sio mwanamke wangu kabisa, alinihakikisha kwamba hataki hata maEx wake wakati ananivisha pete,” Bibi Warda alisema.
Ajuza huyo alisema kuwa baada ya kumshinikiza, kijana huyo alikubali kuwa alichepuka na kumtaka kila mmoja kuondoka kujishughulisha na ya kwake.
“Tumekuwa kwenye mahusiano kwa kama miaka 3 hivi lakini ikaja kujulikana baadae, watoto wangu wanajua, wazazi wake pia wanafahamu sisi ni wapenzi. Niliongea hadi na mamake na akatupa ruhusa. Mamake mimi ni mkubwa kwake kiumri. Lakini hela mimi ninazo, za kuchezea zipo,” aliongeza.
Nyanya huyo alisema kwamba baada ya kuachana, hata hakumpokonya kitu chochote alichomfanyia kijana huyo na kusema kwamba licha ya hayo bado anahisi kidogo yupo moyoni.
Kijana huyo alipoingia studioni, alipigwa na bumbuazi kumkuta bibi huyo studioni lakini alishikilia msimamo wake kwamba hakuchepuka bali video hiyo ilikuwa imehaririwa kuonesha kuwa sura ni yake kumbe si kweli.
