logo

NOW ON AIR

Listen in Live

KBC yafichua sababu ya kutopeperusha mechi ya Harambee Stars baada ya kulaumiwa na waziri Namwamba

Namwamba alieleza kiini cha tatizo lililofanya mechi hiyo kutorushwa na kuwaomba radhi mashabiki wa soka wa Kenya kwa niaba ya kituo hicho.

image
na Radio Jambo

Habari17 November 2023 - 08:33

Muhtasari


•Wasimamizi wa KBC wamewaomba radhi Wakenya na kueleza kuwa walishindwa kupeperusha mechi hiyo kufuatia changamoto ya kiufundi ya satelaiti.

• “Tuna deni la Wakenya la ombi la msamaha wa dhati, usio na shaka na usio na utata kwa kukatishwa tamaa huku," Waziri Namwamba alisema.

wakifanya mazoezi kabla ya mchuano dhidi ya Gabon.

Shirika la utangazaji la kitaifa la Kenya, KBC limetoa taarifa kuwaomba radhi wananchi kwa kushindwa kutangaza moja kwa moja mechi kati ya Harambee Stars na timu ya taifa ya Gabon siku ya Alhamisi usiku.

Mashabiki wengi wa kandanda wa Kenya walikuwa tayari wamewasha runinga zao mwendo wa saa moja usiku wa Alhamisi wakisubiri kufurahia mechi hiyo ya kufuzu kwa Kombe la Dunia la FIFA ambayo ilichezewa jijini Franceville, Gabon lakini walikata tamaa kwani haikuonyeshwa kamwe.

Katika taarifa ya Ijumaa asubuhi, wasimamizi wa KBC waliwaomba radhi Wakenya na kueleza kuwa walishindwa kupeperusha mechi hiyo kufuatia changamoto ya kiufundi ya satelaiti.

"Tunaomba radhi kwa Wakenya kwa kushindwa kupeperusha mechi ya kufuzu kwa Kombe la Dunia la FIFA la 2026 kati ya Gabon na Kenya mnamo Novemba 16, 2023 saa moja usiku kutokana na changamoto ya kiufundi ya satelaiti," wasimamizi wa KBC walisema katika taarifa.

Shirika hilo la utangazaji la serikali ya Kenya hata hivyo limewahakikishia wakenya kuwa wataweza kutazama mechi zijazo za Harambee Stars kwani tatizo hilo limerekebishwa.

"Tafadhali kumbuka kuwa hii imerekebishwa na tunatazamia matangazo bila kukatizwa katika siku zijazo," taarifa hiyo ilisoma.

KBC ilitoa msamaha huo punde tu baada ya waziri wa Michezo na Sanaa Ababu Namwamba kulaumu runinga hiyo inayomilikiwa na serikali kwa kukosa kupeperusha mechi hiyo.

Waziri huyo katika taarifa yake alieleza kiini cha tatizo lililofanya mechi hiyo kutorushwa na kuwaomba radhi mashabiki wa soka wa Kenya kwa niaba ya kituo hicho.

"Jana usiku @KBCChannel1 iliwaangusha mashabiki wa Kenya kwa matatizo ya satelaiti ambayo yalisababisha kushindwa kuonyesha mechi ya Harambee Stars dhidi ya Gabon jijini Franceville," waziri Ababu Namwamba alisema katika taarifa yake Ijumaa asubuhi.

 Aliongeza, “Tuna deni la Wakenya la ombi la msamaha wa dhati, usio na shaka na usio na utata kwa kukatishwa tamaa huku. Hakika mnastahili bora zaidi. POLENI SANA.”

Kwa bahati mbaya, timu ya taifa ya Kenya haikufanikiwa kupata pointi hata moja nchini Gabon kwani ilichapwa mabao 2-1 na mwenyeji.

Masoud Juma aliiweka mbele Harambee Stars katika kipindi cha kwanza baada ya kufunga bao katika dakika ya 40. Hata hivyo, mabao mawili, ya Denis Bouanga na ya Guelor Kanga katika kipindi cha pili yaliwapa wenyeji ushindi mwishoni mwa mechi hiyo ngumu.


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved