Ni pigo jingine kwa rais Ruto na serikali ya Kenya Kwanza baada ya mahakama ya juu jijini Nairobi kupiga breki kwa muda agizo la uzinduzi wa vitambulisho vipya vya kidijitali.
Itakumbukwa wiki chache zilizopita, Ruto alitangaza kuwa serikali yake itazindua vitambulisho vya kidijitali kwa jina Maisha Card kuanzia Desemba lakini mahakama imesitisha utekelezwaji wa agizo hilo hadi kesi itakaposikilizwa na kuamuliwa Februari 6 mwaka 2024.
Jaji John Chigiti aliiamuru serikali kutosajili watu wala kutoa vitambulisho vya kizazi kipya baada ya ombi lililowasilishwa na Taasisi ya Katiba kuonekana kuwa na umuhimu.
"Likizo hii itafanya kazi kwa kukaa, kuzuia utekelezaji au utekelezaji zaidi na mtu yeyote wa uamuzi wa mlalamikiwa wa Novemba 1, 2023 wa kuzindua au kuendesha Maisha Namba, ikiwa ni pamoja na kadi ya kidijitalii, kitambulisho cha kidijitali, kitambulisho cha kipekee cha kibinafsi, na Sajili kuu ya kitaifa ya Idadi ya Watu, kabla na bila tathmini ya athari ya ulinzi wa data kwa mujibu wa Kifungu cha 31 cha Sheria ya Ulinzi wa Data," Jaji Chigiti aliamuru.
Hili ni pigo la tatu katika siku za hivi karibuni kwa uongozi wa Ruto mahakamani.
Itakumbukwa wiki jana mahakama iliamuru kwamba ushuru wa 1.5% kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za bei nafuu ni haramu lakini ikaagiza kwamba utaendelea kutozwa hadi mapema mwakani kesi hiyo itakaposikilizwa na kuamuliwa.
Jumatatu pia, mahakama iliagiza mchakato wa kubinafsishwa kwa taasisi na mali ya serikali kusitishwa katika kesi ambayo iliwasilishwa na Raila Odinga kupitia chama chake cha ODM.
