Mbunge wa Molo ambaye pia ndiye mwenyekiti wa kamati ya fedha kwenye bunge Kimani Kuria ameelezea kilichochochea serikali kupendekeza ushuru wa 16% kwenye bidhaa ya mkate.
Akizunguza kwenye runinga ya Citizen usiku wa Alhamisi, Kuria alisema kwamba serikali iliangalia na kubaini kwamba bidhaa za mkate husababisha ugonjwa wa kisukari na kama njia moja ya kupunguza ugonjwa huo, waliona ni heri kuweka ushuru huo.
Mwenyekiti huyo wa Kamati ya Fedha hata hivyo alikubali hisia zilizoenea miongoni mwa Wakenya kwamba mkate si bidhaa ya kujistarehesha bali ni bidhaa kuu ya chakula inayotumika katika karibia kila boma kila siku.
"Tulikuwa na mazungumzo marefu sana na Hazina ya fedha kuhusu VAT hii. Mawazo ya awali yalikuwa kwamba kuna wasiwasi kuhusu ugonjwa wa kisukari. Hoja tunazopokea kutoka kwa Wakenya ni kwamba mkate si kitu cha kujistarehesha. Watu wanatumia kila asubuhi kwa kiamsha kinywa,” alisema Kimani.
Mbunge huyo alisisitiza kwamba ushuru huo haujaanza kufanya kazi bali ni pendekezo tu na ni jukumu la Wakenya kujitokeza kutoa maoni yao kabla ya mswada wa kifedha wa 2024 haujafikisha bungeni.
"Tumepokea pendekezo hili na tunawauliza Wakenya nini maoni yao kulihusu. Kama kamati, tutapima maoni ya Hazina dhidi ya yale ambayo Wakenya wanasema kabla ya kufanya uamuzi unaofaa kuhusu pendekezo hilo na athari zake,” aliongeza.
Ushuru wa VAT kwenye mkate unapendekezwa kuongezwa kutoka 0% hadi 16% katika mswada wa kifedha wa 2024.
