logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Mbunge Babu Owino amfariji Rigathi Gachagua baada ya kutimuliwa

“Viongozi hukumbana na matatizo mara kwa mara. Ni mzigo ambao sote tunaubeba uongozini,” Babu Owino alisema.

image
na Samuel Maina

Habari19 October 2024 - 08:42

Muhtasari


  • Katika ujumbe wake kwa Rigathi Gachagua, mbunge huyo wa Embakasi Mashariki alibainisha kuwa masaibu yaliyompata mbunge huyo wa zamani wa Mathira ni changamoto ambazo viongozi wote hupitia
  • "Yeye na familia yake wapate amani na ufanisi sasa na katika miaka ijayo," alisema.

Mbunge wa Embakasi Mashariki Paul Ongili almaarufu Babu Owino mnamo Ijumaa jioni alituma ujumbe maalum wa faraja kwa aliyekuwa Naibu Rais wa Kenya Rigathi Gachagua kufuatia kuondolewa kwake afisini.

Alhamisi jioni, bunge la seneti la Kenya liliidhinisha kutimuliwa kwa naibu rais baada ya kuunga mkono mashtaka mbalimbali yaliyotolewa dhidi yake katika hoja iliyowasilishwa na Mbunge wa Kibwezi Magharibi Mwengi Mutuse.

Katika ujumbe wake kwa Rigathi Gachagua, mbunge huyo wa Embakasi Mashariki alibainisha kuwa masaibu yaliyompata mbunge huyo wa zamani wa Mathira ni changamoto ambazo viongozi wote hupitia.

“Viongozi hukumbana na matatizo mara kwa mara. Ni mzigo ambao sote tunaubeba uongozini,” Babu Owino alisema kupitia akaunti yake ya Twitter.

Kiongozi huyo wa zamani wa SONU aliendelea kumtakia naibu wa rais huyo aliyetimuliwa ahueni ya haraka huku akiendelea kupata matibabu hospitalini.

"Yeye na familia yake wapate amani na ufanisi sasa na katika miaka ijayo," alisema.

Aliongeza, "Wakenya wenzangu tuendelee na ujenzi wa taifa na vita dhidi ya ufisadi na kutokujali."

Msimamo wa Babu Owino katika kutimuliwa kwa Rigathi Gachagua umesalia kuwa kitendawili kwani yeye ni miongoni mwa wabunge waliokosa kufika bungeni wakati wa mijadala ya kumng'atua naibu rais na upigaji kura. Pia amekuwa kimya kuhusu suala hilo zima na kuwaacha Wakenya wakiwa na shauku ya kutaka kujua msimamo wake.

Maseneta mnamo  Alhamisi usiku waliunga mkono kuondolewa kwa Naibu Rais Rigathi Gachagua.

Maseneta waliidhinisha mashtaka matano kati ya 11 yaliyotolewa dhidi ya Gachagua.

"Seneti imeazimia kumuondoa afisini kwa kumwondoa madarakani MHE. Rigathi Gachagua, Naibu Rais wa Jamhuri ya Kenya. Kwa hiyo, H.E. Rigathi Gachagua akoma kushikilia wadhifa huo,” Spika Amason Kingi alisema.

Mashtaka yaliyoidhinishwa ni pamoja na; shtaka la maoni ya Wanahisa, mashtaka manne ya kuingilia Uhuru wa Majaji na mashtaka matano ya Sheria ya Uwiano na Uadilifu wa Kitaifa.

Pia walishikilia misingi ya sita na tisa kuhusu uhalifu chini ya Sheria ya Uwiano wa Kitaifa na Utovu wa Maadili Mkubwa.




RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved