logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Si poa watu kutafuta wapendwa wao kwa siku 40 na unasema unajadili uchumi – CS Muturi

“Kama tunawateka nyara na kuwaua Watoto, sasa ni nani tunajadilia uchumi huo? Suala hili linastahili kushughulikiwa na uharaka unaostahili,” aliongeza.

image
na MOSES SAGWEjournalist

Habari31 January 2025 - 14:00

Muhtasari


  • “Nafikiri ni wakati sasa nchi iweke kando shughuli zingine zozote na kuelekeza nguvu katika suala la utekaji nyara na mauaji ya kinyama,” Muturi alisema.

WAZIRI wa utumishi wa umma Justine Muturi kwa mara nyingine tena ameonekana kulenga mkuki wake kwenye kifua cha serikali haswa akikosoa vikali mauaji ya waliotekwa nyara.


Akizungumza katika hifadhi ya maiti ya City alipofika kwa ajili ya vijana wawili kati ya watatu waliotekwa nyara Mlolongo mwishoni mwa mwaka jana na baadae kupatikana wakiwa maiti, Muturi alisema kwamba ni jambo la kusikitisha sana kwa vijana hao kupatikana maiti.


Waziri huyo alisisitiza kwamba si jambo la kufurahisha kuona juhudi za wiki kadhaa za kuwatafuta vijana hao kuishia kwenye hifadhi ya maiti.


Waziri huyo alisema kwamba ni wakati wa taifa kwa jumla kuweka pembeni shughuli zozote zinazoendelea ili kuelekeza nguvu na juhudi katika kuangazia suala la utekaji nyara ambalo limekuwa gumzo la kitaifa katika miezi ya hivi karibuni.


“Nafikiri ni wakati sasa nchi iweke kando shughuli zingine zozote na kuelekeza nguvu katika suala la utekaji nyara na mauaji ya kinyama,” Muturi alisema.


Alisisitiza kwamba licha ya kuwepo ndani ya serikali, hana Habari yoyote kama kunayo kanuni yoyote inayounga mkono utekaji nyara wa aina yoyote.


Muturi alisema kwamba si jambo la kufurahisha kuona wazazi wakiwatafuta wapendwa wao kwa Zaidi ya siku 40 na mtu Fulani ameketi mahali akiwaambia kuhusu kutafuta utatuzi wa suala la kiuchumi.


“Si poa kwamba wazazi wanaweza kukaa kwa kipindi cha Zaidi ya siku 40 kuwatafuta wanao wapendwa na tunaketi mahali tukidai kwamba tunajadili masuala ya uchumi wa nchi, uchumi kwa nani?” Muturi alihoji.


“Kama tunawateka nyara na kuwaua Watoto, sasa ni nani tunajadilia uchumi huo? Suala hili linastahili kushughulikiwa na uharaka unaostahili,” aliongeza.


Tamko la Waziri huyo linajiri siku moja tu baada ya miili ya vijana wawili kati ya 3 waliotekwa nyara Mlolongo – Justus Mutuma na Martin Mwau kupatikana katika makafani ya City.



RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved