logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Homa Bay: Baba Akamatwa Akishukiwa Kumuua Bintiye, 7, Kwa Kumnywesha Petroli

Mwili wa mtoto huyo ambaye ni mwanafunzi wa darasa la pili, ulipatikana ukioza nyumbani kwao Jumanne asubuhi ukiwa na chupa tupu ya petroli kando yake.

image
na MOSES SAGWEjournalist

Habari06 February 2025 - 08:35

Muhtasari


  • Kamanda wa Polisi wa Kaunti Ndogo ya Ndhiwa John Losia alisema mshukiwa ambaye alitoweka alijisalimisha katika Kituo cha Polisi cha Homa Bay baada ya kutekeleza uhalifu huo.
  • Losia alisema wenzake huko Homa Bay walimpigia simu na kumjulisha kuwa kuna mtu alijiwasilisha kwao.



Mwanamume atiwa mbaroni na polisi Homa Bay kwa tuhuma za kumuua mwanawe kwa kumnywesha petroli

MWANAMUME mwenye umri wa miaka 38 katika kaunti ya Homa Bay ametiwa mbaroni na maafisa wa polisi akishukiwa kumuua bintiye mwenye umri wa miaka 7 kwa kumlazimisha kunywa petroli.


Kwa mujibu wa Ripoti za polisi, mwanamume huyo alitenda unyama huo wa kutisha Jumatatu jioni nyumbani kwake katika Kaunti Ndogo ya Ndhiwa.


Mwili wa mtoto huyo ambaye ni mwanafunzi wa darasa la pili, ulipatikana ukioza nyumbani kwao Jumanne asubuhi ukiwa na chupa tupu ya petroli kando yake.


Bado haijabainishwa ikiwa dutu ya petroli ilikuwa na sumu.


Kamanda wa Polisi wa Kaunti Ndogo ya Ndhiwa John Losia alisema mshukiwa ambaye alitoweka alijisalimisha katika Kituo cha Polisi cha Homa Bay baada ya kutekeleza uhalifu huo.


Losia alisema wenzake huko Homa Bay walimpigia simu na kumjulisha kuwa kuna mtu alijiwasilisha kwao.


"Wenzangu huko Homa Bay walinipigia simu kuniambia kuwa mwanamume mmoja alidai kwamba alimuua mtoto wake katika eneo la Kanyikela, karibu na Sukari Industry. Niliwaambia wamzuilie ili maafisa wetu waende huko kwa sababu kulikuwa na uwezekano mkubwa kuwa yeye ndiye tuliyekuwa tukimtafuta,” Losia aliambia vyombo vya habari.


Losia aliwatuma maafisa wake katika Kituo cha Polisi cha Homa Bay na kumpeleka mshukiwa katika Kituo cha Polisi cha Ndhiwa baada ya kuidhinishwa kuwa ndiye mshukiwa wa mauaji ya mtoto huyo.


"Tuligundua kuwa yeye ndiye baba wa msichana aliyekufa. Tumempeleka Kituo cha Polisi Ndhiwa kwa mahojiano zaidi. Tutampeleka mahakamani,” Losia alisema.


Loisa alisema uchunguzi wa awali unaonyesha mtuhumiwa alimlazimisha bintiye marehemu kunywa lita moja ya petroli.



RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved