
Aliyekuwa Gavana wa Kiambu Waititu amekimbizwa katika Hospitali ya Kitaifa ya Kenyatta (KNH) kutokana na matatizo ya shinikizo la damu.
Haya yanajiri siku moja tu baada ya kuhukumiwa kifungo cha miaka 12 au kulipa faini ya Sh52.5 milioni kufuatia kukutwa na hatia katika kesi ya ufisadi ya Sh588 milioni.
Katika hukumu hiyo katika Mahakama ya Milimani mnamo Alhamisi, Waititu vile vile alizuiwa kuwania kiti chochote cha kisiasa kwa kipindi cha miaka 7.
Alishtakiwa pamoja na mkewe, Susan Ndung'u, ambaye alihukumiwa kifungo cha mwaka mmoja au kulipa faini ya Sh500,000.
Mahakama iliwatia hatiani kwa mashtaka yanayohusiana na ufisadi lakini ikawaachilia kwa makosa matatu ya utakatishaji fedha.
Mshtakiwa mwenzao, mkurugenzi wa Testimony Enterprises Limited Charles Chege, pia amepigwa faini ya Sh295 milioni au kutumikia kifungo cha miaka 9 jela.
Beth Wangeci, mkurugenzi wa pili katika Testimony Enterprises Limited pia alitozwa faini ya Ksh.1 milioni au kutumikia kifungo cha mwaka mmoja jela.
