
Rais William Ruto amepata mapokezi ya kishindo katika siku yake ya kwanza ya ziara ya wiki nzima katika eneo la Mlima Kenya, huku maelfu ya wakazi kutoka Laikipia na Nyeri wakionekana kufurahia ziara yake.
Mamia ya wakazi waliovalia vazi la kitamaduni la Kikuyu na mavazi ya kiraia walijipanga, wakisubiri ziara ya rais katika eneo hilo, iliyoanza Jumanne.
Hii ni, licha ya miezi kadhaa ya uasi kutoka eneo hilo, uliosababishwa na kuondolewa afisini kwa aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua.
Rais alipeleka vita hadi mlangoni kwa aliyekuwa naibu wake katika Kaunti ya Nyeri, ambapo aliahidi kurejesha upendeleo kwa wakazi wa Mlima Kenya kwa kumpeleka Ikulu baada ya kukita kambi Kieni na Naromoru.
"Kura yenu ndiyo tumetumia kuunda serikali hii. Kwani nyinyi mnadhani mimi ni mwendawazimu nikasahau? Maneno ya Nyeri katika serikali hii, mtu wa kuulizwa namba moja ni mimi, na nitahakikisha barabara zenu lazima zijengwe, stima iwekwe, maji itengenezwe, soko ijengwe," alisema Ruto.
Naibu wake, Prof. Kithure Kindiki alisema, "Kuna watu wengine kazi yao ni kuanzia kuanzia asubuhi mpaka mchana..."
Rais ambaye alipata takriban kura milioni 3 kutoka kwa kaunti 10 zenye kura nyingi za Mlima Kenya, alimshutumu naibu wake wa zamani kwa kupanda mbegu za mifarakano na ukabila.
"Na mtu asiwaambie sijui kuna njama ya kubagua sijui nani. Hii Kenya hakuna tena siasa itaendeshwa ya ubaguzi, ama chuki, ama ukabila, ama kutenga watu wengine," alisema.
"Wale walikuwa wanani-advice waachane na mimi, I'm not available. Mimi niko kazi," Kindiki alisema
Baadhi ya wafuasi shupavu wa aliyekuwa Naibu Rais, akiwemo Gavana wa Nyeri Mutahi Kahiga na mbunge wa Kieni Njoroge Wainaina, ambaye alibatilisha sahihi yake ya kumfukuza Gachagua ofisini, walidokeza kuruka meli, wakiahidi kufanya kazi na utawala.
"Tulikuwa tumekumiss kidogo... Tuliona haukuji, tukashindwa kwani takwimuje? Hii serikali si yetu? Sasa tukae tuangalie wengine wakikula?" Kahiga aliuliza.
"Na sababu saa zingine mimi husema kama mbaya, leo nataka niseme amefanya vizuri kutuletea maendeleo." Mbunge Wainaina, aliongeza, “Mgeni njoo, mwenyeji apone… Mmetokea vile tulipangana juzi?”
Hapo awali, rais alizindua miradi kadhaa katika kaunti hizo mbili, ikiwa ni pamoja na miradi ya ujenzi wa nyumba za bei nafuu, masoko ya thamani ya zaidi ya shilingi bilioni moja, na mradi wa usambazaji wa umeme vijijini wa Sh720 milioni katika Kaunti ya Laikipia. Pia aliahidi kuunganishwa zaidi kwa kaya 10,000 katika Kaunti ya Nyeri.