logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Kama walidhani kunifuta ndio kuninyamazisha, basi wamebofya wrong namba - Muturi

“Lakini nathubutu kusema hivi, kama lengo [la kufutwa] lilikuwa ni kuninyamazisha, kwa bahati mbaya wamebofya nambari tofauti. Kwa sababu siwezi choka kupigania haki za watu wa hii Jamhuri."

image
na MOSES SAGWEjournalist

Habari02 April 2025 - 14:44

Muhtasari


  • Mara si moja, Muturi amekuwa akiinyooshea serikali kidole cha lawama kuhusu suala la utekaji nyara, akidai kwamba asasi za kiusalama zimekuwa zikihusika.
  • “Hakuna siri kwamba nilifutwa kutokana na msimamo wangu mkali dhidi ya utekaji nyara na mauaji na kile ambacho kimeitwa kususia vikao vya baraza la mawaziri,” Muturi alisema.

Justin Muturi, waziri wa zamani

ALIYEKUWA waziri wa utumishi wa umma Justin Muturi amevunja kimya chake, takribani wiki moja baada ya kufutwa kutoka kwa baraza la mawaziri.

Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari, Muturi alidai kwamba anajua fika sababu iliyopelekea kibarua chake kuota nyasi katika serikali ya rais William Ruto.

Mwanasheria mkuu wa zamani wa serikali alisema kwamba huenda kufutwa kwake kulichochewa na misimamo yake mikali ambayo amekuwa nayo dhidi ya utekaji nyara.

Mara si moja, Muturi amekuwa akiinyooshea serikali kidole cha lawama kuhusu suala la utekaji nyara, akidai kwamba asasi za kiusalama zimekuwa zikihusika.

“Hakuna siri kwamba nilifutwa kutokana na msimamo wangu mkali dhidi ya utekaji nyara na mauaji na kile ambacho kimeitwa kususia vikao vya baraza la mawaziri,” Muturi alisema.

Hata hivyo, spika huyo wa zamani wa bunge la kitaifa alisema kwamba kama rais Ruto alidhani kumfuta ndio njia ya kumnyamazisha, basi ameula wa chuya.

Aliapa kuendeleza misururu ya mashambulidi dhidi ya serikali na kuitaka iwajibikie kile alichokitaja kuwa matendo yao maovu dhidi ya wananchi.

“Lakini nathubutu kusema hivi, kama lengo [la kufutwa] lilikuwa ni kuninyamazisha, kwa bahati mbaya wamebofya nambari tofauti. Kwa sababu siwezi choka kupigania haki za watu wa hii Jamhuri, bila kujali gharama yake,” Muturi alisema.

Hotuba yake inakuja siku moja tu baada ya kukabidhi mamlaka ya ofisi aliyekuwa akiishikilia kwa waziri mwenye mamlaka makuu, Musalia Mudavadi.

Rais Ruto juzi akizungumza na wanahabari kutoka eneo pana la Mlima Kenya kuelekea mwanzo wa ziara ya siku 5 ya kimaendeleo katika eneo hilo, aligusia kuondolewa kwa Muturi katika baraza la mawaziri.

Ruto alisema kwamba Muturi alijifuta kazi mwenyewe kwani alianza kususia vikao vya baraza la mawaziri, akisema kwamba hata kuondoka kwake hakutamuathiri pakubwa kwani bado ana pesheni kama spika mstaafu.

Ruto alitangaza mabadiliko kwenye baraza lake la mawaziri wiki jana ambapo alimteua mbunge wa Mbeere Kaskazini Geoffrey Ruku kuchukua nafasi ya Justin Muturi katika wizara ya utumishi wa umma.

Makala Zinazohusiana


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved