
Rais William Ruto ametangaza mipango ya kupandisha hadhi ya mji wa Meru kuwa jiji, hatua itakayoufanya kuwa jiji la tano nchini Kenya baada ya Nairobi, Mombasa, Kisumu na Nakuru.
Tangazo hilo lilitolewa Jumamosi alasiri wakati wa mkutano wa hadhara katika eneo la Makutano, Kaunti ya Meru.
Akihutubia umati uliokuwa na shauku, Ruto alisema ukuaji wa kasi wa Meru na uwezo wake mkubwa wa kiuchumi umeifanya kuwa mgombea thabiti wa hadhi ya jiji. Aidha, aliahidi uwekezaji mkubwa wa miundombinu ili kusaidia mabadiliko hayo.
“Gavana amesema anataka Meru iwe jiji lijalo la Kenya. Mnataka Meru iwe jiji lijalo? Kwa hivyo mnafikiri mimi sikuwa na hiyo wazo? Tayari nilikuwa nayo akilini,” alisema Ruto, akivutia shangwe kutoka kwa umati.
Ili kuimarisha maendeleo ya Meru, Rais alitangaza kuwa serikali kuu itatoa Shilingi bilioni 2 kwa ujenzi wa masoko ya kisasa 16 katika maeneo mbalimbali ya kaunti hiyo.
Masoko hayo mapya yanatarajiwa kuimarisha biashara na kuinua maisha ya wakazi katika kaunti hiyo inayotegemea kilimo kwa kiasi kikubwa.
Katika agizo alilotoa papo hapo, Ruto alimpa Waziri wa Maji na Usafi wa Mazingira, Eric Mugaa, jukumu la kuhakikisha mfumo wa majitaka wa kaunti hiyo unaboreshwa kikamilifu kufikia Desemba mwaka huu — hatua muhimu kuelekea hadhi ya jiji.
“Miradi hii haihusu tu miundombinu; inahusu kuunda mazingira ya kuvutia uwekezaji, kusaidia biashara na kuinua ubora wa maisha,” alisema Rais.
Hatua hiyo imekuja kufuatia ombi rasmi kutoka kwa Gavana wa Meru, Isaac Mutuma, ambaye alimtaka Rais kutambua umuhimu unaokua wa Meru kama kitovu cha kiuchumi na idadi ya watu katika eneo hilo.
“Shida yetu kubwa ilikuwa mfumo wa majitaka wa Meru, lakini sasa utakamilika ili jiji lijalo nchini Kenya liwe Meru. Tunataka jiji lijalo liwe safi mara tu mfumo huo utakapokamilika,” alisema Gavana Mutuma.
Juhudi za Meru kupata hadhi ya jiji zinafanana na safari ya Nakuru, iliyofikia kilele chake mwaka 2021 baada ya kuidhinishwa na Seneti.
Kulingana na Sheria ya Maeneo ya Mijini na Majiji ya Kenya, mji unapaswa kuwa na idadi ya watu isiyopungua 250,000, mpango wa maendeleo ya mji unaofanya kazi, na uwezo wa kifedha wa kudumisha huduma za kiwango cha jiji ili kustahiki hadhi hiyo.