
Waziri wa zamani wa Utumishi wa Umma na Maendeleo ya Rasilimali Watu, Justin Muturi, amesema anajutia uamuzi wake wa kujiunga na kambi ya kisiasa ya Rais William Ruto.
Kauli yake imekuja siku chache baada ya kusema kuwa atamheshimu daima Rais mstaafu Uhuru Kenyatta.
Muturi alisema kuwa Uhuru alikuwa kiongozi madhubuti lakini wa haki, aliyekuwa msikivu, aliyekubali maoni tofauti na aliyeongoza bila woga.
“Nitamheshimu daima Rais mstaafu Uhuru Kenyatta. Alikuwa kiongozi madhubuti lakini wa haki, aliyesikiliza, aliyekubali maoni yanayotofautiana na hakuongoza kwa hofu. Bado ni rafiki yangu hadi leo, na ninathamini uhusiano huo,” alisema Muturi.
Muturi alisisitiza kuwa bado ni marafiki hadi sasa. Hata hivyo, alieleza majuto yake kwa kumuunga mkono Rais Ruto, akisema alifanya kosa kubwa.
“Lakini ninajutia sana kumuunga mkono William Ruto,” aliandika kupitia ukurasa wake wa X.
Haya yanajiri miezi michache baada ya kufutwa kazi kutoka katika Baraza la Mawaziri.
Wakati wa utawala wa Uhuru, Muturi alihudumu kama Spika wa Bunge la Kitaifa kwa kipindi cha miaka 10. Baadaye alihamia upande wa Ruto, ambaye wakati huo alikuwa Naibu Rais, katika kipindi cha kuelekea uchaguzi mkuu wa 2022.
Ruto alishinda uchaguzi huo na kumteua Muturi kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Muturi aliingia kwenye mzozo na Ruto licha ya kuhudumu katika serikali yake kwa takriban miaka miwili, kwanza kama Mwanasheria Mkuu na baadaye kama Waziri wa Utumishi wa Umma.
Mvutano huo ulianza baada ya mwanawe Muturi kutekwa nyara wakati wa maandamano makali ya kizazi cha Gen Z nchini.
Muturi alidai kuomba hatua zichukuliwe kutoka kwa Baraza la Mawaziri kukomesha utekaji nyara na mauaji ya kiholela, na hata akaacha kuhudhuria vikao vya baraza hilo.
Alisema aliandika barua kwa Rais kuhusu suala hilo. Waziri huyo wa zamani alidai kuwa alijaribu kuomba msaada wa Rais ili mwanawe aachiliwe baada ya kutekwa.
Alidai kusikia mazungumzo ya simu kati ya Rais na Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Ujasusi wa Kitaifa, na baada ya hapo, mwanawe aliachiliwa.
Tangu aondoke serikalini, Muturi amekuwa akishirikiana na viongozi wa upinzani wakiwemo Naibu Rais wa zamani Rigathi Gachagua, Makamu wa Rais wa zamani Kalonzo Musyoka, Martha Karua, Eugene Wamalwa na wengine.