
Seneta mteule wa UDA, Karen Nyamu, amewaonya vijana dhidi ya kutumiwa na viongozi wanaojitakia makuu ambao hawako tayari kuruhusu serikali ifanye kazi zake kwa amani.
Kupitia ukurasa wake wa Facebook siku ya Alhamisi, Karen alieleza kushangazwa kwake na maandamano ambayo yalipaswa kuwa ya kuheshimu maisha ya vijana waliopigania mageuzi, lakini yakageuka kuwa machafuko.
“Maandamano ya jana sijapenda. Nilidhani ni memorial tukumbuke wale waliuawa last year. Lakini ikakua ni vurugu, vitisho na tension mob. Kwa nini? Nyinyi mlipenda?” aliuliza.
Aliyataja maandamano ya Jumatano kuwa hayakuwa na maana, akieleza kuwa uharibifu ulioshuhudiwa uliwasababishia hasara kubwa baadhi ya wafanyabiashara.
“Wakati huu unaweza kusema walikuwa waandamanaji wapya bila mwelekeo. Ilikua strategy yenu ama mlifuata script ya nani?
“Biashara nyingi ziliumia, nyingi zikiwa zinaendeshwa na Wakiuyu wangu wachapa kazi. Yuko wapi yule msemaji wa kujiteua wa Wakikuyu kulaani haya mambo?”
Aliwataka vijana kujiepusha na viongozi ambao ajenda yao kuu ni kuingiza nchi katika vurugu.
Akitumia mfano wa mpenzi wake wa zamani, ambaye alimkataza kuwa na uhusiano mwingine baada ya kuachana, Karen alidai kuwa baadhi ya viongozi wanawivu na wanaotawala sasa, na wako tayari kufanya lolote kuwaangamiza.
“Jihadharini na viongozi ambao hawana cha kupoteza. Viongozi waliopoteza kila kitu ikiwemo dhamira yao. Nilikuwa na ex aliyeniambia, kama siwezi kuwa na wewe basi hakuna mwingine atakayekuwa na wewe. Kama siwezi kuwa kiongozi Kenya, basi hakuna mwingine anayefaa kuwa,” alisema.