
Kiongozi wa chama cha Wiper Democratic Movement, Kalonzo Musyoka, amesema ana uwezo wa kumshinda Rais William Ruto katika uchaguzi wa urais wa mwaka 2027.
Akizungumza Alhamisi, Juni 26, 2025, wakati wa mahojiano na kituo kimoja cha runinga cha humu nchini, Kalonzo alisema ni wazi kuwa Ruto hawezi kumshinda endapo watakutana katika kinyang’anyiro huru na haki.
“Hii ni wazi kabisa bana, sitaki ata kuharibu wakati. Hakuna hata mtoto ambaye ameanza kupata maarifa mwenye hajui atakaye kabiliana vilivyo na William Ruto kama hatakuwa amejiuzulu, kwa uchaguzi ujao, ni Steven Kalonzo Musyoka. Hiyo ni wazi,” alisema Kalonzo.
Kalonzo aliongeza kuwa atawasikiliza wenzake katika upinzani, kufanya mazungumzo nao na kushirikiana nao kwa kila njia ili kuhakikisha ushindi katika uchaguzi huo.
Hata hivyo, alikanusha uwezekano wa kushirikiana tena na kiongozi wa chama cha Orange Democratic Movement (ODM), Raila Odinga, akisema kuwa waziri mkuu huyo wa zamani anapaswa kuruhusiwa kustaafu kwa heshima.
Aidha, Kalonzo alisema kuwa nia yake kwa kipindi kilichosalia ni kushirikiana na viongozi wenzake wa upinzani ili kurejesha taifa katika mkondo uliokusudiwa na waasisi wa taifa.
“Na hiyo sio kumaanisha kwamba sitasikiza wenzangu. Tutafanya mazungumzo, tutafanya kila tunaloweza, na Raila Odinga namheshimu, astaafu kwa heshima zake. Kwa kipindi ambacho kimesalia, nia yangu pamoja na wenzangu ni tushirikiane turejeshe taifa hili mahali ambapo waanzilishi walikuwa wananuia,” alisema.