
Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen ameagiza maafisa wa polisi kumpiga risasi mtu yeyote atakayejaribu kuvamia kituo cha polisi.
Akizungumza baada ya kukagua uharibifu katika Kituo cha Polisi cha Dagoretti kufuatia maandamano ya Juni 25, Murkomen aliwaambia wakazi kwamba amewaagiza maafisa wapige risasi yeyote atakayevamia vituo vya polisi kuanzia sasa.
“Tumeambia polisi wampige risasi yeyote anayekaribia kituo cha polisi,” alisema Murkomen.
Agizo la Murkomen halikupokelewa vyema na wakazi waliokuwa wakimzomea na kumkosoa vikali.
Baadhi ya wakazi walisikika wakipiga kelele kwa kutumia kauli ya ‘wantam’, ambayo hutumiwa na viongozi wa upinzani katika kampeni dhidi ya kuchaguliwa tena kwa Rais William Ruto.
Licha ya kuzomewa na umati wenye hasira, Murkomen alisisitiza agizo lake, akisema watu wanaojaribu kuiba bunduki kutoka kwa polisi hawapaswi kuchukuliwa kwa mzaha.
“Mtu anayejitahidi kuiba bunduki, anajaribu kung’oa bunduki kutoka kwa afisa wa polisi… unafikiri mtu kama huyo atakamatwa tu? Haiwezekani… mtu anayerusha mawe kwa polisi, unafikiri atatendewa kwa upole?” aliuliza.
Katika mkutano na wanahabari awali, Murkomen alitangaza kuwa bunduki tano ziliibiwa katika Kituo cha Polisi cha Dagoretti wakati wa maandamano ya Jumatano.
“Wahalifu walilenga maafisa waliokuwa kazini. Walikuwa wakilenga bunduki katika bohari pamoja na sare za polisi. Bunduki tano ziliibiwa katika Kituo cha Polisi cha Dagoretti, Kaunti ya Kiambu, huku bunduki nyingine nne zikichomwa katika Kituo cha Polisi cha Gachui na wahalifu hao hao waliokuwa wakijificha nyuma ya kivuli cha maandamano ya amani,” Murkomen alisema.
Kutokana na hilo, Waziri huyo wa Usalama wa Ndani alitangaza kuwa maafisa wa upelelezi watawafuatilia wahusika.
Alizielezea maandamano ya Juni 25 kama jaribio la mapinduzi, akidai kuwa baadhi ya wanasiasa walihusika katika kupanga na kuajiri wahuni kwa ajili ya maandamano hayo.