
Maafisa wa usalama waliokuwa wakilinda aliyekuwa Jaji Mkuu David Maraga wameondolewa siku chache tu baada ya yeye kujiunga na waandamanaji katika jiji la Nairobi mnamo Juni 25, 2025.
Akizungumzia suala hilo kupitia barua rasmi kwa Inspekta Jenerali wa Polisi na Wizara ya Mambo ya Ndani na Utawala wa Kitaifa, iliyochapwa tarehe 27 Juni, Maraga alisema kuwa kuondolewa kwa walinzi wake kunahusiana na ukosoaji wake wa wazi kwa uongozi wa polisi nchini.
Alisema kuwa mmoja wa walinzi wake aliagizwa kutofika kazini mnamo Juni 25, bali aende kufanya rekodi ya kawaida katika sajili ya silaha.
"Mnamo Juni 25, siku ambayo niliungana na vijana pamoja na familia za wahanga waliopoteza maisha au kupotea kutokana na matukio ya mwaka mmoja uliopita, mmoja wa maafisa waliokuwa wamenkabidhiwa kazi ya kunilinda aliambiwa asifike kazini bali aende kufanya rekodi ya kawaida ya kila mwezi kwenye sajili ya silaha," alisema.
Maraga aliongeza kuwa mnamo Juni 26, alifahamishwa kuwa maafisa wengine waliokuwa wakimlinda waliagizwa kuripoti vituoni mwao.
"Alipowasili asubuhi hiyo, aliambiwa ghafla kuwa kulikuwa na mafunzo yaliyopangwa kufanyika siku hiyo hiyo. Siku iliyofuata, yaani Juni 26, niliarifiwa kuwa maafisa wengine wa usalama waliokuwa wakinilinda waliagizwa kuripoti vituoni mwao bila taarifa zaidi," barua hiyo inasoma.
Alisisitiza kuwa bado ana haki ya kupewa ulinzi na msaada mwingine kutoka kwa Huduma ya Kitaifa ya Polisi kama sehemu ya mafao ya kustaafu ya Jaji Mkuu.
Maraga alisema kuwa tangu kustaafu kwake mnamo Januari 2021, amekuwa akihudumiwa na walinzi wenye silaha kwa mujibu wa masharti ya sheria hiyo.
"Kwa mujibu wa sheria, aliyekuwa Jaji Mkuu anastahili kupewa ulinzi wa polisi pamoja na madereva, ambao hutolewa kwa maombi ya Jaji Mkuu mstaafu," aliongeza.
Aliitaka mamlaka husika kurejesha ulinzi wake mara moja. Pia alihoji jinsi polisi wanavyoshughulikia hali tata nchini na kuihimiza Wizara ya Ndani kuchunguza suala hilo.
"Kwa msingi huo, nataka ulinzi wangu urejeshwe mara moja," aliandika.
Maraga si kiongozi pekee aliyeshiriki maandamano ambaye ulinzi wake umeondolewa.
Mnamo Juni 26, Mbunge wa Embakasi Mashariki, Babu Owino, alitangaza kuwa ulinzi wake umeondolewa baada ya kushiriki maandamano ya Juni 25.
Mbunge wa Embakasi Mashariki, Babu Owino, wakati wa maandamano katika jiji la Nairobi siku ya Jumatano, Juni 25, 2025.