
Kiongozi wa ODM Raila Odinga amesema alikataa mwaliko kutoka kwa viongozi wa upinzani waliotaka awasaidie kupinga utawala wa Rais William Ruto.
Raila alidai kuwa viongozi hao wa upinzani waliahidi kuunga mkono azma yake ya urais kama angekubali kushirikiana nao kuipinga serikali.
Akizungumza katika eneo la Rarieda jana, kiongozi huyo wa ODM alisema kuwa ameazimia kushirikiana na Rais William Ruto.
“Siendi popote. Sitamwacha Ruto kwa sababu najua tunakoelekea. Tutatembea pamoja kwa mshikamano hadi tufikie tulipoelekea,” aliongeza.
“Watu wengine walisema sisi ni wageni... Hao ndio hao hao waliodai kuwa kama hukuwapigia kura, basi huna hisa. Mmoja wao hata alisema kuwa akitupata kwenye foleni ya kuelekea Ikulu, atatutoa. Je, unaweza kweli kufanya kazi na mtu kama huyo?” alihoji.
Waziri Mkuu wa zamani alisema hakuna mtu anayeweza kudai kuwapa wafuasi wake mwelekeo wa kisiasa, akisema kuwa wakati ufaao ukifika, yeye mwenyewe atatoa mwelekeo.
Aliwakosoa wale aliowataja kuwa wameanza kampeni za mapema, akisisitiza kuwa huu si wakati wa siasa.
Aliwaambia wafuasi wake kuwa ni busara kila wakati kutafuta njia za kukabiliana na wapinzani wa kisiasa.
“Tumechukua hatua ya ujasiri sana kwa kushirikiana na serikali ya Kenya Kwanza. Hatuna haja ya kukaa au kuwaacha watu wetu wakikaaa gizani kila wakati. Kila tunapopata fursa inayoweza kubadilisha maisha ya watu wetu, huitumia,” alisema.
Alisema kuwa uamuzi wa kushirikiana na Rais Ruto haujamzuia yeye na wafuasi wake kusonga mbele.
Aliandamana na Waziri wa Nishati Opiyo Wandayi, ambaye alisema kuwa Raila amewapa idhini ya kufanya kazi na kuiunga mkono serikali ya Kenya Kwanza.
Wandayi, ambaye alilaani maandamano ya kumbukumbu ya Juni 25, alisema kuwa ilikuwa njama ya upinzani kuleta vurugu nchini.
Aliwalaumu wakosoaji wa serikali, ambao alidai kuwa na nia ya kuleta mkanganyiko nchini.