
Niliwaonya Kuhusu Ruto Mkanipuuza— Uhuru Kenyatta
Onyo Larejea Tena
NOW ON AIR
Rais Ruto asema wakati wa Ukambani kubaki upinzani umeisha
Muhtasari
MAKUENI, KENYA, Jumatano, Novemba 12, 2025 – Rais William Ruto ameapa kuhakikisha kwamba eneo la Ukambani halitakaa tena upande wa upinzani, akisema wakati wa kisiasa wa kugawanyika umefika mwisho.
Akizungumza mjini Kibwezi, kaunti ya Makueni, wakati wa uzinduzi wa miradi ya maendeleo, Ruto alisema serikali yake iko tayari kufanya kazi kwa karibu na wananchi wa Ukambani kuhakikisha wanapata nafasi katika ajenda kuu ya taifa.
“Kwa vyovyote vile, mbele na nyuma, kulia na kushoto, juu na chini — hii Ukambani haiwezi tena kukaa upinzani,” alisema Ruto huku umati ukishangilia.
Rais alikiri kuwa amechangia kwa sehemu kubwa eneo hilo kubaki nyuma kisiasa, akisema kuwa alipuuza Ukambani katika miaka iliyopita na kuwaruhusu wapinzani wake “kuwapotosha wananchi.”
“Ni kweli, niliacha pengo, na wale wapinzani wangu wakaingia. Lakini sasa nimefika, na nimeamua Ukambani lazima iungane na serikali,” alisema Ruto huku akipigiwa makofi.
Alisema kuwa ana dhamira ya dhati ya kuunganisha taifa lote kupitia maendeleo, na si kwa misingi ya upinzani au mirengo ya kisiasa.
Rais Ruto pia alitumia jukwaa hilo kuwashambulia wapinzani wake, akisema hawana dira wala mpango wa maendeleo kwa wananchi.
“Mtu kama hana mpango, sera, agenda au akili atabadilisha Ukambani namna gani? Atabadilisha namna gani?” aliuliza huku umati ukijibu kwa kelele za “Asante Ruto!”.
Aliongeza kuwa watu wa Ukambani wanahitaji huduma za msingi kama maji safi, barabara bora, umeme, na ajira — mambo ambayo, kwa maneno yake, yanaweza kutekelezwa tu na serikali yenye mipango na uwajibikaji.
Rais alikosoa baadhi ya viongozi wa upinzani kwa “kukosa sera na kushikilia maneno ya kisiasa yasiyo na faida.”
“Niliwaonya zamani, mkikaa mkirudia maneno kama ‘one-term’, ‘Kasongo’ au ‘must go’, hamtapata kura ya hawa wananchi. Wamechoka na kelele, wanataka matokeo,” alisema.
Ruto pia aliwashutumu baadhi ya wanasiasa kwa “kushindania kugawana serikali” badala ya kushirikiana katika kuleta maendeleo halisi.
“Badala ya kushindania viti, tushindanie nani ataleta miradi mingi zaidi kwa wananchi,” alisisitiza.
Ruto, akiwa ameandamana na Naibu Rais Kithure Kindiki, mawaziri kadhaa na viongozi wa Ukambani, alianza ziara ya siku nne katika kaunti za Makueni, Kitui na Machakos.
Katika ziara hiyo, Rais anatarajiwa kufungua miradi kadhaa ikiwemo ujenzi wa barabara za Kibwezi–Makindu, mradi wa maji wa Thwake, na usambazaji wa umeme vijijini.
“Miradi hii sio ya ahadi tena. Ni miradi ya vitendo. Tunataka kila nyumba iwe na umeme, maji na barabara zinazopita,” alisema.
Ruto aliwataka wananchi wa Ukambani kushirikiana na serikali ili kufanikisha ajenda ya maendeleo ya taifa, akisema serikali yake haitatenga mtu yeyote.
“Ukambani ni sehemu muhimu ya Kenya. Bila Ukambani, maendeleo ya nchi hii hayata kamilika,” alisema.
Aidha, Ruto aliahidi kuimarisha uwekezaji katika kilimo cha umwagiliaji na kuanzisha viwanda vya kuchakata mazao ya wakulima ili kuongeza kipato.
Ziara ya Rais Ruto Ukambani inatarajiwa kubadilisha mwelekeo wa kisiasa wa eneo hilo, huku akiweka wazi nia yake ya kuhakikisha hakuna Wakenya wanaosalia nyuma kimaendeleo kwa sababu ya misimamo ya kisiasa.

Onyo Larejea Tena
Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7
© Radio Jambo 2024. All rights reserved