Jukwaa la Hong Ting lilifanyika Alhamisi jijini Nairobi, mji mkuu wa Kenya, na kuwakutanisha maafisa wa serikali, wasomi na watendaji wa vyombo vya habari kujadili mbinu bunifu za kuendeleza uboreshaji wa kisasa wa China-Afrika katika kipindi cha miaka mitano ijayo.
Liliandaliwa na Taasisi ya Historia ya Chama na Fasihi ya Kamati Kuu ya Chama cha Kikomunisti cha China na Shirika la Habari la Xinhua, chini ya kaulimbiu “Fursa na Changamoto kwa China na Afrika Kuendeleza Uboreshaji wa Kisasa Pamoja katika Miaka Mitano Ijayo.”
Qing Xuemin, mkurugenzi wa Idara ya Sita ya Utafiti katika taasisi hiyo, alisema jukwaa hilo lilikuwa muhimu katika kuimarisha ushirikiano kati ya China na Afrika, unaojengwa juu ya kuaminiana, kuheshimiana na matokeo ya kunufaishana pande zote.
“Ushirikiano wa China na Afrika unalenga kujenga jumuiya ya China-Afrika ya kudumu katika nyakati zote yenye mustakabali wa pamoja kwa zama mpya, ili marafiki zetu wa Afrika nao wanufaike na matunda ya maendeleo,” alisema Qing, akibainisha kuwa katika miaka ya hivi karibuni China imeendelea kuwa mshirika mkubwa zaidi wa kibiashara wa Afrika na imewekeza pakubwa katika miundombinu, huduma za afya, elimu na teknolojia za kidijitali barani humo.
Qing alisema kuwa utoaji wa msamaha wa ushuru wa sifuri kwa asilimia 100 ya bidhaa kwa nchi 53 za Afrika zilizo na uhusiano wa kidiplomasia na China unatarajiwa kufufua biashara kati ya China na Afrika. Aliongeza kuwa ushirikiano wa hali ya juu chini ya Mpango wa Ukanda na Njia (Belt and Road Initiative) utaongeza kasi ya uboreshaji wa kisasa wa miundombinu, kilimo na viwanda barani Afrika.
Peter Kagwanja, mkurugenzi mkuu wa Taasisi ya Sera za Afrika (Africa Policy Institute), taasisi ya tafiti ya Kiafrika yenye makao yake Nairobi, alisema msukumo wa China katika uboreshaji wa kisasa umekuwa chanzo cha msukumo kwa nchi za Kusini mwa Dunia, nyingi zikiwa barani Afrika. Alisema mafanikio ya China katika kupunguza umaskini na utawala wa ngazi ya jamii yamekuwa funzo kwa mataifa ya Afrika katika juhudi zao za kutengeneza njia zao za maendeleo zinazotokana na mazingira yao wenyewe.
“Uboreshaji wa kisasa wa aina ya ndani ya nchi, unaotofautiana kulingana na historia, utamaduni na mazingira ya kiuchumi ya kila nchi, unaobadilisha jamii za jadi, vijijini na za kilimo kwa ubora na kwa wingi kuelekea jamii za juu zaidi, za mijini na za kiviwanda,” alisema Kagwanja.
Hassan Khannenje, mkurugenzi wa Taasisi ya Kimataifa ya Mafunzo ya Kimkakati ya HORN (HORN International Institute for Strategic Studies), taasisi ya tafiti yenye makao yake Nairobi, alisema historia ya karne nyingi ya uhusiano wa China na Afrika inaandikwa upya kwa kuzingatia zaidi “programu laini” ikiwemo uhamishaji wa ujuzi na teknolojia, kubadilishana tamaduni na maendeleo ya kijani.
“Fursa katika kipindi cha miaka mitano ijayo si tu kuimarisha uhusiano wa Afrika na China, bali ni uhusiano wa uboreshaji wa kisasa unaounda mustakabali wa uchumi wa dunia,” alisema Khannenje.
Peter Kagwanja, mkurugenzi mkuu wa Taasisi ya Sera za Afrika, akizungumza wakati wa Jukwaa la Hong Ting jijini Nairobi, Kenya, Desemba 4, 2025. Jukwaa la Hong Ting liliwakutanisha maafisa wa serikali, wasomi na watendaji wa vyombo vya habari kujadili mbinu bunifu za kuendeleza uboreshaji wa kisasa wa China-Afrika katika kipindi cha miaka mitano ijayo. (Xinhua/Yang Guang)
Hassan Khannenje (kushoto), mkurugenzi wa Taasisi ya Kimataifa ya Mafunzo ya Kimkakati ya HORN, akizungumza wakati wa Jukwaa la Hong Ting jijini Nairobi, Kenya, Desemba 4, 2025. (Xinhua/Yang Guang)
Qing Xuemin, mkurugenzi wa Idara ya Sita ya Utafiti katika Taasisi ya Historia ya Chama na Fasihi ya Kamati Kuu ya Chama cha Kikomunisti cha China, akizungumza wakati wa Jukwaa la Hong Ting jijini Nairobi, Kenya, Desemba 4, 2025. (Xinhua/Yang Guang)

