Picha ya ndege isiyo na rubani iliyopigwa Mei 9, 2026 inaonyesha meli ya mizigo ikiwasili katika Bandari ya Qingdao mjini Qingdao, Mkoa wa Shandong mashariki mwa China. (Picha na Yu Fangping/Xinhua)
Katika miaka ya hivi karibuni, uhusiano kati ya China na Marekani umepitia misukosuko mbalimbali. Baadhi ya wachambuzi wana hofu kuwa China na Marekani zinaweza kurudia historia ya ushindani wa mataifa makubwa unaojulikana kama “Mtego wa Thucydides.”
Hata hivyo, Rais wa China Xi Jinping amepinga wazo hilo: “Hakuna kitu kinachoitwa ‘Mtego wa Thucydides’ duniani. Lakini makosa ya mara kwa mara ya kimkakati kati ya mataifa makubwa yanaweza kujitengenezea mtego huo.”
Kwa hivyo, kuepuka makosa hayo ya kimkakati limekuwa jukumu muhimu kwa China na Marekani, jambo linalohitaji pande zote mbili kushiriki mazungumzo ya wazi kuhusu masuala kadhaa muhimu.
Kwanza ni suala la Taiwan. Rais Xi mara kadhaa ameueleza wazi upande wa Marekani msimamo wa msingi wa China. Katika mazungumzo ya simu ya Februari 4 na Rais wa Marekani Donald Trump, Xi alisisitiza tena kuwa suala la Taiwan ndilo nyeti zaidi na muhimu zaidi katika uhusiano wa China na Marekani, akiitaka Marekani kushughulikia mauzo ya silaha kwa Taiwan kwa umakini mkubwa.
Biashara ni suala jingine muhimu. Katika kukabiliana na mashambulizi ya ushuru wa forodha ya upande mmoja kutoka Marekani, China chini ya uongozi wa Xi imechukua hatua madhubuti za kujibu.
Wakati huohuo, Beijing imeendelea kuweka wazi njia za mazungumzo. Xi ametuma timu za uchumi na biashara ambazo zimefanya duru sita za mazungumzo na upande wa Marekani, kwa lengo la kupunguza tofauti hatua kwa hatua huku wakipanua maeneo ya makubaliano ya pamoja. Kwa sasa, uhusiano wa kibiashara kati ya nchi hizo mbili umeendelea kuwa thabiti kwa kiasi kikubwa. Pande hizo mbili zitafanya duru mpya ya mazungumzo ya biashara nchini Korea Kusini kuanzia Mei 12 hadi 13.
Rais wa China Xi Jinping akitoa hotuba katika hafla ya chakula cha jioni iliyoandaliwa na mashirika rafiki nchini Marekani, mjini San Francisco, Marekani, Novemba 15, 2023. (Xinhua/Yao Dawei)
Katika mkutano wao wa Busan, Xi alisisitiza umuhimu wa kuwa na mtazamo mpana katika kushughulikia migogoro hiyo. “Pande zote mbili zinapaswa kuwa na mtazamo mpana na wa muda mrefu,” Xi alimwambia Trump, “zikizingatia faida za kudumu za ushirikiano badala ya kuingia katika mzunguko mbaya wa kulipizana kisasi.” Trump alimwelezea Xi kama kiongozi mkubwa na mzungumzaji mwenye msimamo thabiti.
Je, Xi anaonaje mustakabali wa uhusiano wa pande hizo mbili? Katika hotuba aliyotoa mjini San Francisco mwaka 2023, aliuliza kile alichokiita swali muhimu zaidi: “Je, sisi ni maadui au washirika?”
“Ikiwa upande mmoja utauona mwingine kama mshindani mkuu, changamoto kubwa zaidi ya kisiasa duniani na tishio la kimkakati,” alionya, “hali hiyo itasababisha sera zisizo sahihi, hatua zilizopotoshwa na matokeo yasiyotakiwa.”
Xi pia alisisitiza kuwa China haina nia ya kuipinga au kuiondoa Marekani katika nafasi yake. “China kamwe haiweki dau dhidi ya Marekani,” alisema. “Vivyo hivyo, Marekani haipaswi kuweka dau dhidi ya China.”
Kutokana na uzoefu wa uhusiano wa China na Marekani, Xi ameweka wazi misingi mitatu — kuheshimiana, kuishi kwa amani na ushirikiano wa manufaa kwa wote — kama njia sahihi ya kusonga mbele kwa mataifa hayo mawili.
