Xi Jinping na Aleksandar Vucic wakishiriki kwa pamoja hafla ya kutiwa saini nyaraka za ushirikiano baada ya mazungumzo yao mjini Beijing, Mei 25, 2026. (Xinhua)Wakati Rais wa Serbia, Aleksandar Vucic, akiendelea na ziara yake ya kiserikali nchini China, mataifa hayo mawili yanatarajiwa kuimarisha zaidi ushirikiano wao wa kimkakati wa pande zote.
Kwa wasafiri kati ya mji mkuu wa Serbia, Belgrade, na mji wa pili kwa ukubwa nchini humo, Novi Sad, muda wa safari umepungua kutoka saa moja na nusu hadi dakika 30 pekee kutokana na reli ya kisasa ya mwendo kasi iliyojengwa na kampuni ya China.
Kwa wafanyakazi wa Kiwanda cha Chuma cha Smederevo Steel Plant, uwekezaji wa China umefufua kiwanda hicho cha kihistoria na kubadilisha maisha ya maelfu ya watu.
Rais wa China, Xi Jinping, amekuwa akielezea urafiki kati ya China na Serbia kama “wa chuma usiovunjika.”
Kufufua viwanda vya jadi
Kilichoanzishwa mwaka 1913, Kiwanda cha Chuma cha Smederevo kilikuwa kikijulikana kama “fahari ya Serbia.” Hata hivyo, kufikia mwishoni mwa miaka ya 1990 kilikabiliwa na changamoto za ushindani na usimamizi hafifu, hali iliyokisogeza karibu na kufungwa.
Mwaka 2016, HBIS Group ilinunua kiwanda hicho. Mwaka huo huo, Xi alikitembelea kiwanda hicho na kuwahakikishia wafanyakazi kwamba kingefufuliwa.
Kwa mujibu wa mfanyakazi mkongwe Nenad Cvetanovic, uwekezaji huo ulileta utulivu na matumaini mapya kwa wafanyakazi waliokuwa wakikabiliwa na hali ya kutokuwa na uhakika kuhusu mustakabali wao.
Kupitia juhudi za pamoja, kiwanda hicho sasa kimerudi kuwa moja ya nguzo kuu za mauzo ya nje ya Serbia.
Hadithi kama hiyo pia imeonekana katika mji wa madini wa Bor, ambapo shughuli za uchimbaji zilizokuwa zimeelemewa na madeni zilifufuliwa baada ya uwekezaji mkubwa wa Zijin Mining Group. Hatua hiyo imeisaidia Bor kuwa miongoni mwa miji yenye ustawi mkubwa na mishahara ya juu zaidi nchini Serbia.
Katika kipindi cha miaka 10 iliyopita, uwekezaji wa China nchini Serbia umefikia mabilioni ya dola za Marekani, na kuifanya China kuwa mojawapo ya vyanzo vikuu vya uwekezaji wa moja kwa moja kutoka nje.
Aidha, kuongezeka kwa upatikanaji wa soko la China kumeongeza fursa kwa bidhaa za Serbia kama vile mvinyo, asali, nyama ya ng’ombe na kondoo. Takwimu zinaonyesha kuwa mauzo ya Serbia kwenda China yaliongezeka kutoka dola milioni 22 mwaka 2013 hadi dola bilioni 1.9 mwaka 2024.
Kuimarisha miundombinu ya usafiri
Mnamo Oktoba 2025, sehemu ya Serbia ya reli ya Budapest-Belgrade Railway ilifunguliwa kikamilifu, hatua iliyoboreshwa kwa kiasi kikubwa muunganiko wa usafiri katika eneo hilo.
Mtafiti mwandamizi wa Taasisi ya Siasa za Kimataifa na Uchumi ya Serbia, Aleksandar Mitic, alisema reli hiyo imeleta mabadiliko makubwa katika maisha ya kila siku ya wananchi.
Mbali na reli, barabara kuu na njia za haraka zilizojengwa na kampuni za China zimepunguza muda wa safari, kuunganisha miji na jamii mbalimbali na kurahisisha shughuli za kiuchumi.
Faida hizo pia zimeonekana katika sekta ya utalii. Kwa mujibu wa Marija Labovic, Mkurugenzi wa Shirika la Kitaifa la Utalii la Serbia, watalii wa China walirekodi zaidi ya usiku 85,000 wa malazi nchini Serbia katika robo ya kwanza ya mwaka 2026.
Kufungua maeneo mapya ya ushirikiano
Katika mazungumzo yake na Vucic, Xi alisema China na Serbia zinapaswa kupanua ushirikiano katika sekta zinazoibuka kama akili mnemba (AI), uchumi wa kidijitali, nishati safi na viwanda vya kisasa.
Baada ya mazungumzo hayo, viongozi hao walishuhudia kutiwa saini kwa zaidi ya nyaraka 20 za ushirikiano katika nyanja za siasa, biashara, sayansi na teknolojia, elimu, sheria na utamaduni.
Kwa mujibu wa taarifa ya pamoja iliyotolewa Jumatatu, pande hizo mbili zitafanya kazi ya kuoanisha Mpango wa 15 wa Miaka Mitano wa China (2026–2030) na Mkakati wa Maendeleo wa Serbia 2030.
Wakati wa ziara yake Beijing, Vucic pia alitembelea kiwanda cha Xiaomi na kujaribu gari la umeme la kampuni hiyo.
Miradi mipya ya ushirikiano tayari inaendelea kutekelezwa, ikiwemo ujenzi wa kiwanda cha roboti katika mji wa Sabac na mradi wa nishati ya upepo katika mji wa Pancevo.
Aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Yugoslavia, Zivadin Jovanovic, alisema ushirikiano wa kimkakati kati ya China na Serbia unalenga kuboresha maisha ya wananchi wa nchi hizo mbili.
Aliongeza kuwa uwekezaji wa China umechangia ukuaji mkubwa wa uchumi wa Serbia huku ukitoa njia mbadala kwa masharti ya kisiasa na kifedha ambayo mara nyingi huambatana na taasisi za Magharibi.




