Familia ya aliyekuwa mpenzi wa Noti Flow, Armaan Bux almaarufu King Alami imeendelea kuomba msaada wa fedha za kugharamia bili yake ya hospitali.
King Alami amekuwa akipokea matibabu maalum katika Hospitali ya Kitaifa ya Kenyatta kwa siku kadhaa zilizopita baada ya kupata majeraha mabaya mwilini..Alivunjika viungo kadhaa vya mwili na kupata majeraha baada ya kudaiwa kuruka kutoka kwenye jengo la ghorofa mapema mwezi huu.
Katika taarifa iliyotolewa na babake na kushirikishwa na Noti Flow kwenye mitandao ya kijamii, Alami amelazimika kufanyiwa upasuaji mara kadhaa baada ya ajali hiyo katika juhudi za kuokoa maisha yake.
"Hamjambo, familia ya Arman Bux inaomba usaidizi wenu katika kutafuta pesa za kulipa bili za matibabu. Arman ni binti ya Shakay na Sakina Bux ambaye hivi majuzi alianguka vibaya na kuachwa na majeraha makubwa yaliyohitaji kufanyiwa upasuaji mara kadhaa. Madaktari wamelazimika kukata mkono mmoja na wanaendelea na kazi," sehemu ya taarifa ya babake Alami ilisoma.
Rapa Noti Flow aliwaomba Wakenya kuendelea kumchangia mpenzi huyo wake wa zamani na kuiombea familia yake.
Ripoti kadhaa zilidai kwamba Alami alianguka kutoka kwa jengo la ghorofa mwishoni mwa wiki iliyopita. Noti na Alami walikuwa wametengana siku kadhaa tu kabla ya tukio hilo la kutisha kutokea..
Rapa huyo amekuwa akilaumiwa na baadhi ya Wakenya ambao wanaamini alihusika katika suala hilo huku wengine wakiamini Alami alikumbwa na msongo wa mawazo baada ya wawili hao kutengana.
Siku kadhaa zilizopita Noti alisema lawama hizo zimemfanya ajisikie kuwa mkosaji na kuweka wazi kuwa yuko tayari kubeba lawama akibainisha kwamba Alami angekuwa sawa iwapo wangekuwa pamoja.
"Kwa wale wanaonilaumu, asanteni sana kwa kunifanya nijisikie vibaya na kuwa na hatia zaidi kuliko nilivyo tayari. Wote mko sahihi, ni kosa langu kwa sababu ningekuwa naye angekuwa sawa na salama kama yeye. kila mara imekuwa ikinisulubisha sana,” aliongeza.
Rapa huyo amewaomba Wakenya kuheshimu ufaragha wa familia ya mpenzi huyo wake wa zamani katika kipindi hiki kigumu.
