Wakenya kwenye mtandao wa Facebook wamempongeza MC na mwimbaji maarufu wa nyimbo za Injili za Kikuyu, Karangu Muraya baada ya kuwapeleka likizo binti zake wawili kutoka kwa uhusiano wake wa awali.
Katika chapisho lake la Facebook la Ijumaa asubuhi, mwanamuziki huyo mwenye utata alifichua kuwa wasichana hao wawili walikuwa wakielekea likizo, kwa hisani ya kampuni maarufu ya utalii ya Expeditions Maasai Safaris.
Alitumia posti hiyo kuelezea upendo wake mkubwa kwa binti zake na pia kumshukuru Mkurugenzi Mtendaji wa Expeditions Maasai Safaris, Bw Pancras Karema kwa likizo hiyo.
"Nendeni mkafurahie likizo yenu wasichana wangu,.. baba yenu anawapenda," Bw Karangu Muraya aliandika Ijumaa asubuhi.
Aliambatanisha taarifa yake na picha za mabinti hao wawili warembo wakipanda kwenye ndege ambayo ilikuwa iwapeleke mahali pa likizo.
"Kwa kaka yangu Pancras Karema wa Expeditions Maasai Safari, asante kwa kuwapa likizo wasichana wangu, ninashukuru sana," aliongeza.
Wanamitandao wengi wameonekana kufurahishwa na kitendo cha mwanamuziki huyo kuwatambua na kuwasherehekea pia watoto aliozaa na mpenzi wake wa awali.
Idadi kubwa ya mashabiki kwenye Facebook walimtambua kama baba mzuri huku wengine wengi wakizungumzia jinsi walivyofurahishwa na hatua hiyo.
Tazama maoni ya baadhi ya wanamtandao;-
Jacinta Kuria: Wewe ni baba mkubwa. Mungu akubariki kwa kuwatunza binti zako.
Purity Macharia: Wow.. Nimeipenda hii.
Essy wa willy official: Baba mzuri anajulika na vitendo.. mimi wangu anazurura tu hata hakumbuki ana watoto, ni vizuri kwanza mtu awe anaangalia anazaa na kina nani.
Kairetu ka Wanjira: Wewe ni baba mzuri.
Pendo Jean: Heko Mr Wonderful, Mungu akubariki sana, wewe ni madini adimu.
Hatua ya mwanamuziki Karangu Muraya na Expedition Maasai Safari kuwapeleka likizo wasichana hao wawili likizoni inajiri siku chache tu baada ya kampuni ya utalii inayoongozwa na mtaalamu wa utalii Pancras Karema kuwapeleka likizo mke wa sasa wa mwanamuziki huyo na watoto wao watatu katika eneo la Pwani.
Katika siku kadhaa za hivi majuzi, mwimbaji huyo wa nyimbo za injili amekuwa akionyesha picha nzuri za familia yake wakifurahia wakati mzuri jijini Mombasa na katika bahari la Hindi baada ya kutunukiwa likizo ya siku kadhaa.


