Mwimbaji wa nyimbo za injili za Kikuyu Mary Lincoln ameungama dhambi za na kutubu baada ya picha zake chafu kusambaa kwenye mitandao ya kijamii wiki iliyopita.
Mnamo Jumatatu, Lincoln ambaye ni mke wa mtangazaji maarufu wa Kikuyu Njogu wa Njoroge aliitisha mkutano wa maombi ambapo kundi la wachungaji lilimwombea.
Mkutano huo wa maombi ambao uliofanyika katika kanisa la CFF Kiambu ulipeperushwa moja kwa moja kwenye YouTube na mitandao mingine ya kijamii. Askofu wa kanisa hilo Bishop Michael Wanderi ndiye aliongoza ibada hiyo.
"Asante Mungu kwa upendo wenu. Bishop Wanderi na Rev David Mwangi Mungu awabariki 🙏 Shiru Wa Gp Kenya ,Joyce Irungu The Bosslady, Karangu Muraya, Anne Lawrence, Judie Masila, Wairimu Muchiri na wasanii wenzangu wote na marafiki wote ambao wamekuwa wakisali nami, asanteni sana," Lincoln alisema baada ya ibada.
Wakati wa ibada, Askofu Wanderi aliomba radhi kutoka kwa Mungu na Wakenya kwa niaba ya Lincoln na kanisa lote kwa jumla.
Aliwahimiza watu kuchukua hatua za ujasiri kama vile kutubu baada ya kutenda dhambi badala ya kuchukua maisha yao.
"Hili ni kosa. Hatutalirudia tena. Tunamuomba Mungu atusamehe kama kanisa. Nasimama hapa kama askofu kuomba msamaha kwa Mungu na kwa watu wote ambao waliona zile picha..Kuna watu kadhaa katika Bibilia ambao walitenda kosa, moja alikuwa Judas. Alimsaliti Yesu lakini hakuchukua njia nzuri kama ile Mary alichukua. Sisi ambao tunajuana na Mungu , ata lifanyike la aina gani, hatuchukui njia ya Judas," alisema.
Mwimbaji Shiru wa GP alizungumza kwa niaba ya wasanii kadhaa ambao walikuwa wamefika katika kanisa hilo kumuunga mkono Lincoln.
Wiki iliyopita baadhi ya picha za utupu zinazodaiwa kuwa za mwimbaji huyo wa nyimbo za injili zilisambaa kwenye mitandao ya kijamii.
Wakenya wengi walijitokeza kumkosoa msanii huyo na kumshutumu kwa unafiki. Hata hivyo, wengine walimtetea wakidai kwamba kila mtu ana mwelekeo wa kufanya dhambi.