logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Jamaa aliyekuwa akiendesha kundi la Telegram la "KCSE 2024 Leakage Group' atiwa mbaroni

Mshukiwa anakabiliwa na mashtaka ya kumiliki vifaa vya mitihani visivyoidhinishwa, kinyume na sheria ya KNEC.

image
na Samuel Maina

Yanayojiri11 November 2024 - 12:34

Muhtasari


  • Imeripotiwa kuwa mshukiwa alikuwa msimamizi wa kundi la "KCSE 2024 Leakage Group" kwenye Telegram ambalo lilitumiwa kwa wizi wa mitihani.
  • Idara ya DCI pia imetangaza kuwa msako mkali unaendelea ili kuwanasa washukiwa zaidi wanaohusika na makosa sawia.


Maafisa wa upelelezi katika eneo la Masaba Kaskazini, kaunti ya Nyamira wanamzuilia mwanamume mmoja wa miaka 25 anayedaiwa kuhusika na makosa ya mitihani.

Kulingana na ripoti ya Kurugenzi ya Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI), mshukiwa Stephen Nyang'au Mbeche alikamatwa siku ya Jumapili, Novemba 10, na maafisa wa upelelezi wa Baraza la Kitaifa la Mitihani la Kenya (KNEC) kwa ushirikiano na maafisa wa eneo la Masaba Kaskazini baada ya operesheni ya ufuatiliaji endelevu.

Imeripotiwa kuwa mshukiwa aliyekamatwa alikuwa msimamizi wa kundi la "KCSE 2024 Leakage Group" kwenye mtandao wa Telegram ambalo lilitumiwa kwa wizi wa mitihani.

"Upekuzi wa kina katika majengo yake ulisababisha kunaswa kwa simu ya rununu na kompyuta ndogo, vifaa vinavyodhaniwa kuwa anatumia kuwahadaa wazazi na wanafunzi waliohusika katika udanganyifu huo," ripoti ya DCI ilisoma.

Kurugenzi pia ilichapisha baadhi ya mazungumzo na karatasi zilizotumwa kwenye kikundi hicho cha Telegraph.

Mshukiwa huyo sasa anatayarishwa kwa ajili ya kufunguliwa mashtaka mahakamani baada ya kukamatwa.

Anakabiliwa na mashtaka ya kumiliki vifaa vya mitihani visivyoidhinishwa, kinyume na sheria ya KNEC.

Idara ya DCI pia imetangaza kuwa msako mkali unaendelea ili kuwanasa washukiwa zaidi wanaohusika na makosa sawia.



RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved