
Kenya inapania kuongeza katika siku za hivi karibuni kufungua vituo vingine vinne vya matibabu ya kansa katika maeneo tofauti tofauti nchini.
Waziri wa afya Deborah Barasa, amesema kuwa serikali itapanua huduma kwa wagonjwa wa saratani kwa kuongeza vituo vya saratani vya kikanda katika kaunti za Kisumu, Kakamega, Meru na Nyeri. Waziri amesema hayo kwenye mkutano wa nane wa mkutano wa kimataifa wa saratani wa Kenya jijini Kisumu.
Kwa mujibu wa waziri Barasa, vituo hivyo vipya vitajiunga na vituo vilivyopo kwa sasa katika kaunti za Nakuru, Mombasa na Garissa ambavyo tayari vinatoa huduma kwa wagonjwa wa saratani.
Kuongezwa kwa vituo hivyo kunalenga kugatuliwa kwa huduma ya matibabu ya kansa, kupunguza msongamano wa wagonjwa kwenye hospitali za rufaa na kuimarisha ufikiaji wa matibabu kwa jamii zote nchini.
Katika hafla hiyo, waziri Baraza amesisitiza kujitolea kwa
serikali katika kudhugulikia ongezeko la ugumu wa matibabu ya saratani kupitia uwekezaji
wa miundombinu sahihi, utambuzi wa ugonjwa huo na ujumuishaji wa huduma chini
ya mpango wa huduma ya afya kwa wote UHC.
Vile vile, Barasa amesema kuwa matibabu ya
saratani yamejumuishwa katika mfuko wa bima ya afya ya jamii chini ya mamlaka ya
afya kwa jamii SHA ili kupunguza mzigo wa kulipia huduma hiyo kwa wagonjwa.
