Mshauri Mkuu katika Baraza la Washauri wa Uchumi wa Ikulu Moses Kuria amekashifu kisa ambapo waombolezaji walizuia kusomwa kwa ujumbe wa rambirambi wa Rais William Ruto wakati wa mazishi ya mwanawe mwanasiasa Lenny Kivuti.
"Katika Utamaduni Wetu, KAMWE hatukatai rambirambi hata kutoka kwa maadui zetu wakubwa. Jumbe husomwa hadharani kwa ajili ya faraja ya familia iliyofiwa. Ndiyo sababu maombi hufanywa hadharani ikiwa ni pamoja na maombi kwa ajili ya familia (Vinginevyo makasisi wangerudi nyuma ya hema na familia na kuomba faraghani,” Kuria alisema.
Waziri huyo wa zamani wa Utumishi wa Umma aliendelea kumtaka Bw Kivuti, ambaye mwanawe alikuwa akizikwa, kujitenga na kile kilichotokea.
“Natarajia Sen Leny Kivuti kujitenga na kitendo hiki kisicho cha kimungu. Sio lazima umpende Rais bali ni HAKI yake kufariji familia,” alisema.
Waziri wa Utumishi wa Umma Justin Muturi alishindwa kusoma ujumbe wa rambirambi wa Rais William Ruto wakati wa mazishi ya mwanawe aliyekuwa Seneta wa Embu Lenny Kivuti, Eric Kivuti siku ya Ijumaa.
Rais hakuweza kuhudhuria ibada hiyo kwa kuwa alikuwa katika mazishi ya mamake Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetangula huko Bungoma.
Hata hivyo, alikuwa ameandika ujumbe wa kusomwa kwa familia na waombolezaji.
Wakati Waziri Muturi aliposimama kusoma ujumbe huo, umati ulianza kupiga kelele, hivyo ikawa vigumu kwake kuendelea. "Nimepewa ujumbe wa rambirambi, kutoka kwa Mheshimiwa Rais... (kelele) Sasa pale nimefika mwisho ni kwamba nimepewa ujumbe. Niwapatie. Nisome ama nisisome?" Muturi aliuliza
Waziri alionekana akimshirikisha Askofu aliyekuwa akiongoza ibada kabla ya kuendelea.
"Nimeshauriwa kwa busara na unajua kama spika wa zamani… na mnajua marehemu JJ Kamotho, aliwahi kusema kuhusu kura ya makelele, nimeskia kura ya makelele.... Niko na heshima kufikisha ujumbe huu kwa Mhe lenny Kivuti hadharani,” alisema.
Muturi alikiri jibu lao, akieleza kuwa alikuwa ameshauriwa kusoma ujumbe huo hadharani.
