Mfanyibiashara maarufu wa Kenya Joseph Wambui almaarufu Khalif Kairo hatimaye amevunja kimya kuhusu kukamatwa kwake na kuhojiwa hivi majuzi.
Katika taarifa yake Jumatatu asubuhi, Kairo ambaye anajulikana sana kwa biashara ya magari na ushawishi wake katika mitandao ya kijamii alithibitisha kuwa siku mbili alikuwa chini ya ulinzi wa polisi.
Kairo alidokeza kuwa kukamatwa kwake kuliibuka kutokana na mzozo wa biashara na mteja ambaye alimshtaki kwa mamlaka.
“Nimetumia siku mbili zilizopita katika kituo cha polisi cha Capitol Hill kama mgeni wa serikali baada ya mabishano yangu siku ya Jumamosi katika polisi wa eneo la Nairobi na afisa wa DCI pamoja na mteja ambaye alikuwa na nia ya kunidhalilisha kwa kurekodi video za kukamatwa kwa siri na kuhojiwa ili kusambazwa kwenye mtandao kupitia wanablogu wa kulipwa,” Kairo alisema.
Mfanyabiashara huyo mwenye umri wa miaka 28 aliendelea kusimulia matukio yaliyojiri baada ya kukamatwa akifichua kuwa atafikishwa mahakamani leo, Jumatatu.
"Nilikataa "kujadili" suluhu ya haraka kama ilivyotarajiwa na badala yake nikasisitiza kuwasilishwa mahakamani leo. Nimevumilia unyanyasaji mkubwa wiki chache zilizopita na licha ya kusisitizwa kwangu kwamba tusuluhishe maswala kwa njia ya haki kwa kutumia taratibu za kiraia, baadhi ya wateja wenye uhusiano wa karibu wamekuwa wakitumia baadhi ya maafisa wa DCI kunikatisha tamaa na kuifanya iwe vigumu zaidi kwetu kufanya biashara na kushughulikia masuala yao ambayo ni za kiraia na zinaungwa mkono na mikataba ya kibiashara,” alisema.
Kairo
pia alikariri kutokuwa na hatia akibainisha kuwa anachopitia ni changamoto
zinazomkumba mfanyabiashara yeyote.
“Mimi si mhalifu lakini mmoja wa wafanyabiashara wengi waaminifu nchini Kenya wanaopitia changamoto kutokana na nyakati ngumu za kiuchumi. Nitafikishwa mahakamani katika mahakama za Milimani muda si mrefu. Nashukuru kwa sapoti kubwa, jumbe za matumaini, maombi na nia njema ambazo nimepokea kutoka kwa umma," alisema.
“Mungu akubariki. Ninasalia imara, nimejitolea kusuluhisha maswala yoyote ambayo hayajashughulikiwa na najua kuwa hii ni hatua ambayo tutashinda kampuni yetu, "aliongeza.
Kairo alikamatwa siku ya Jumamosi huku tetesi zikiibuka kuwa kulikuwa na hali ya kutoelewana kati yake na mteja.
Haikuwa mara ya kwanza kwa mfanyibiashara huyo kijana kukamatwa kwa masuala yanayohusiana na biashara. Mwaka jana alikamatwa tena kwa sababu sawa.